1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yaiwekea vikwazo Mahakama ya ICC

7 Februari 2025

Rais wa Marekani Donald Trump ametia saini amri ya kuiwekea vikwazo Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ICC kutokana na uamuzi wa mahakama hiyo wa kuichunguza Israel ambayo ni mshirika wa karibu wa Marekani.

https://p.dw.com/p/4q9hm

Trump akitia saini moja ya amri zake baada ya kuingia madarakani katika muhula wake wa pili wa uongozi
Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: Picture-Alliance/AP Photo/E. Vucci

Amri ya Rais Donald Trump ya kuiwekea vikwazo Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu, ICC imetolewa Alhamisi ikikishutumu chombo hicho kwa kujihusisha na vitendo visivyo na msingi vilivyo kinyume cha sheria dhidi ya Marekani na Israel.

Zaidi, maelezo katika amri hiyo yameilaumu ICC kwa kutumia vibaya mamlaka yake dhidi ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu kwa kutoa waranti wa kukamatwa  kwake pamoja na aliyekuwa Waziri wake wa Ulinzi, Yoav Gallant.

ICC ilitoa waranti wa kukamatwa kwa wawili hao ikiwatuhumu kwa kuhusika na uhalifu wa kivita kutokana na namna walivyojibu mashambulizi ya Hamas ya Oktoba 7 mwaka 2023. Hata Hivyo, Netanyahu amekuwa akiulalamikia uamuzi huo wa ICC akisema kuwa haukuwa wa haki.

Soma zaidi: Umoja Ulaya waahidi kuwa pamoja na ICC baada ya vikwazo vya Marekani

Amri maalumu iliyosainiwa na Trump dhidi ya ICC Alhamisi imeeleza kwamba Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu haina mamlaka juu ya Marekani na Israel ikizingatiwa kuwa nchi hizo mbili haziitambui mahakama hiyo.

Vikwazo vilivyowekwa na Marekani kupitia amri ya rais dhidi ya ICC vinaweza kujumuisha kuzuia mali na wafanyakazi wa mahakama hiyo pamoja na ndugu zao kuingia Marekani.

Israel yaupongeza uamuzi wa Trump

Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Israel, Gideon Saar kupitia ukurasa wake wa X, ameipongeza hatua hiyo ya Trump akisema vitendo vya ICC vilikuwa sawa na uovu na havikufuata sheria.

Jengo la Mahakama ya ICC mjini The Hague
Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ICCPicha: Alex Gottschalk/DeFodi Images/picture alliance

Mahakama ya ICC kwa upande wake, imelaani amri ya Trump na imeapa kuwa itaendelea kutoa haki na matumaini kwa mamilioni ya watu wanaoathiriwa na ukatili kote duniani. Taarifa ya mahakama hiyo imesema kuwawekea vikwazo maafisa wake kunalenga kuharibu kazi ya mahakama huru isiyo na upendeleo.

Nao Umoja wa Ulaya, leo Ijumaa umeonya kuwa vikwazo vya Marekani dhidi ya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ya ICC vinatishia uhuru wa chombo hicho na mfumo wa sheria.

Halmashauri ya umoja huo katika tamko tofauti limeilaani pia hatua hiyo na kutahadharisha kwamba amri dhidi ya ICC inaweza kuathiri upelelezi na kesi zinazoendelea zikiwemo zinazohusu Ukraine, na kuathiri juhudi za miaka mingi za kuhakikisha kunakuwa na uwajibikaji kote duniani.