1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni: Boris Johnson avuka kura ya kutokuwa na imani naye.

Zainab Aziz Mhariri: Mohammed Khelef
7 Juni 2022

Waziri Mkuu wa Uingereza amevuka kura ya kutokuwa na imani naye lakini siyo kwa kishindo. Kutokana na matokeo Boris Johnson hatakuwa na nguvu za kutosha kama hapo awali. Hayo ni maoni ya mwandishi wa DW Barbara Wesel.

https://p.dw.com/p/4CM6d
Großbritanien I Boris Johnson
Picha: Rob Pinney/Pool/AP/picture alliance

Wapinzani wa waziri mkuu Johnson ndani ya chama chake cha wahafidhina bado wanamwinda. Ujumbe mmoja uko wazi kabisa, kwamba ameponea chupuchupu kwa mara nyingine. Hata hivyo inapasa kutilia maanani kwamba ushindi wake katika kura hiyo ya maoni ulikuwa mdogo kulingalisha na ule wa waziri mkuu wa hapo awali Theresa May, miaka mitatu iliyopita. Hakuna kadhia nyingine itakayomsumbua John kuliko ukweli huo.

Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson
Waziri Mkuu wa Uingereza Boris JohnsonPicha: Matt Dunham/AP Photo/picture alliance

Ushindi wa Johnson unaashiria pia kushindwa. Mifano ya hapo awali ni shubili kwa Waziri Mkuu Boris Johnson. Waziri Mkuu wa hapo awali Theresa May alijiuzulu miezi sita tu baada ya kura ya maoni licha ya kupita katika kura hiyo kwa asilimia takriban 60. Theresa May hakuwa na mashiko tena pia kutokana na njama za Boris Johnson wakati huo. Alilazimika kuachia ngazi kwa ghadhabu.

Waziri mkuu mwingine John Major pia alishinda kura ya kutokuwa na imani naye juu ya mkataba wa Masstricht wa Umoja wa Ulaya mnamo mwaka 1993. Hata hivyo bwana Major alishindwa katika uchaguzi uliofutia. Ishara kwa waziri mkuu Boris Johnson siyo nzuri.

Mbele: Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza Theresa May
Mbele: Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza Theresa May Picha: picture alliance/dpa

Kwa sasa ataepukana na kura hizo kwa muda wa mwaka mzima ujao. Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson ni mtu mahiri katika kukanganya ukweli japo kwa vipindi vifupi. Atazingatia asilimia 59 ya kura alizopata kuwa ni ushindi unaompa mamlaka ya kuendelea kuwamo madarakani. Hata hivyo anapaswa kuizingatia kura hiyo ndani ya chama chake kuwa ni tahadhari.

Au kama alivyosema waziri wake wa masuala ya Brexit Jacob Rees, kwamba hata wingi wa kura moja bado ni wingi. Hivyo ndivyo hasa Boris Johnson mwenyewe anavyotafsiri dunia lakini hilo ni kosa.Ukweli ni kwamba amepoteza uzito maalumu wa kisiasa kutokana na matokeo ya kura hiyo. Rangi imekauka na waziri mkuu Boris Johnson ameathirika. Haijalishi ni kwa muda gani ataendelea kuwamo madarakani ila kwa hali ilivyo, Johnson atachechemea badala ya kutembea haraka.

Waziri Mkuu Boris Johnson akilihutubia bunge baada ya kutolewa ripotui ya Sue Grary.
Waziri Mkuu Boris Johnson akilihutubia bunge baada ya kutolewa ripotui ya Sue Grary. Picha: PRU/AFP

Kama ni kura juu ya tabia yake Johnson ameanguka vibaya. Kilichotifua mambo na kusababisha hali ya kutoridhika miongoni mwa wabunge ni tafrija alizoandaa kwenye ofisi yake wakati wa maambukizi ya virusi vya corona. Mara kadhaa Johnson na  wapambe wake walikiuka taratibu zilizowekwa ili kudhibiti maambukizi ya corona. Hayo yangelitosha kwa  kwa Johnson kujiuzulu au kuondolewa madarakani.

Chanzo:Wesel, Barbara