1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mpango wa kuwapeleka wahamiaji Rwanda ni kinyume cha sheria

15 Novemba 2023

Serikali ya Uingereza imesema leo kuwa bado itajaribu kuwapeleka baadhi ya wahamiaji nchini Rwanda, licha ya uamuzi wa Mahakama ya Juu ya Uingereza kuwa mpango huo tata sio halali kisheria.

https://p.dw.com/p/4Yqwa
Mahakama yaamua kuwapeleka wahamiaji Rwanda, kunawaweka katika hatari ya kuteswa
Moja ya waandamanaji nje ya Mahakama Kuu ya Uingereza akipinga mpango wa kuwapeleka wahamiaji Rwanda Picha: Kirsty Wigglesworth/AP Photo/picture alliance

Waziri mkuu Rishi Sunak na Rais wa Rwanda Paul Kagame wamezungumza leo baada ya uamuzi huo na kusisitiza dhamira yao ya kuufanikisha mpango huo wa uhamiaji.

Sunak amesema uamuzi huo wa mahakama sio matokeo waliyoyataka lakini akaapa kuendelea na mpango huo.

Mahakama Uingereza yabatilisha kupeleka wakimbizi Rwanda

"Wamethibitisha kuwa msingi wa kuwapeleka waomba hifadhi katika nchi ya tatu iliyo salama ni halali kisheria. Kuna vipengele zaidi ambavyo wanataka uhakika zaidi na mabadiliko yaliyobainishwa. Nimebaini kuwa mabadiliko yanaweza kufanywa katika siku zijazo kushughulikia masuala hayo. Serikali tayari imekuwa ikiufanyia kazi mkataba mpya na Rwanda na tutakamilisha hilo kulingana na uamuzi wa leo," alisema Sunak.

Majaji watano wa mahakama ya Juu waliridhia uamuzi wa mahakama ya chini wakisema kuwa waomba hifadhi watakaopelekwa Rwanda watakuwa katika hatari ya kuteswa, kwa sababu wanaweza kurejeshwa nchi walizotokea kama maombi yao ya hifadhi yatakaliwa.