1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mafuriko yaua watu 50 DRC

13 Desemba 2022

Mvua kubwa zasababisha mafuriko na maporomoko ya udongo katika mji mkuu wa DRC Kinshasa ambako mpaka barabara kuu imepasuka vipande viwili

https://p.dw.com/p/4Ksh5
Südafrika Überschwemmungen nach Unwettern
Picha: RAJESH JANTILAL/AFP

Takriban watu 50 wamefariki katika mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo,Kinshasa baada ya mvua kubwa kusababisha mafuriko na maporomoko ya ardhi yaliyosomba makaazi ya watu.

Picha zilizorushwa kwenye mitandao ya kijamii ambazo shirika la habario la Reuters halikuweza kuzithibitisha mara moja zimeonesha maeneo mengi ya mji huo yakiwa kwenye mafuriko na matope huku barabara zikipasuka.

soma pia:Je mabadiliko ya tabia nchi yamechangia mafuriko?

Video moja iliyonesha barabara kuu ya eneo hilo ikipasuka katikati na kuacha shimo kubwa lilosababisha magari chungunzima kutumbikia  katika wilaya ya Mont-Ngafula.

Südafrika | Erdrutsch in Marianridge
Picha: Rogan Ward/REUTERS

Watu waliokuwa karibu wakishuhudia walionekana wakitafuta maeneo ya pembeni kujinusuru.Mkuu wa polisi Sylviano amesema kiasi watu 50 wamefariki kufuatia mafuriko hayo na idadi hiyo inaweza kuongeza.

Waziri mkuu na gavana wa mkoa huo wanatembelea maeneo yaliyokumbwa na mafuriko na maafisa wa eneo hilo wanatarajiwa kukutana na wawakilishi wa wizara ya mambo ya ndani na vyombo vingine vya dola kulishughulikia suala hilo la dharura.

Kinshasa ambao uliwahi kuwa na vijiji vya uvuvi katika ukingo wa  mto Congo umegeuka kuwa moja ya miji mikubwa kabisa ukiwa na wakaazi kiasi milioni 15.

Hata hivyo mifumo mibovu ya mpangilio wa mji huo uliokuwa kwa kasi umeifanya Kinshasa kuzidi kuwa katika hatari ya kukabiliwa na mafuriko baada ya mvua za mfululizo  ambazo zimekuwa zikishuhudiwa mara kwa mara kutokana na mabadiliko ya tabia nchi.

Kiasi watu 39 walifariki mnamo mwaka 2019 kufuatia mvua za msimu zilizosababisha mafuriko katika wila kadhaa za mji huo na baadhi ya majengo kuporomoka barabara kuharibiwa vibaya.

 

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW