1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macron aendeleza juhudi kuzima mzozo Ukraine

Hawa Bihoga
8 Februari 2022

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amezuru mjini Kyiv kuendeleza juhudi za kutuliza mzozo juu ya Ukraine, huku waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani, Annalena Baerbock, akizuru uwanja wa mapambano mashariki mwa nchini hiyo.

https://p.dw.com/p/46hZ8
Ukraine Kiew Besuch Macron
Picha: Thibault Camus/AP/picture alliance

Ziara ya Rais Macron inakuja baada ya mazungumzo na rais wa Urusi Vladmir Putin yaliodumu kwa masaa kadhaa, kumalizika bila muafaka wa dhahiri.

Macron amekutana na rais wa Ukraine Volodymyr Zelensnky, wakati ambapo wasiwasi ukiongezeka juu ya uwezekano wa uvamizi wa Urusi.

Taifa hilo limepeleka wanajeshi zaidi ya 100,000 karibu na mipaka ya Ukraine, lakini linasisitiza kuwa halina mipango ya kuishambulia nchi hiyo.

Kremlin inasema inataka uhakikisho kutoka mataifa ya Magharibi kwamba NATO haitoikubalia uanachama Ukraine na mataifa mengine yaliokuwa sehemu ya Muungano wa Kisovieti, kwamba isitishe uwekaji wa zana za kivita katika eneo hilo, na kuondoa vikosi vyake kutoka eneo la Ulaya Mashariki - madai ambayo Marekani na NATO imeyakataa na kuyataja kuwa yasio na mashiko.

Ukraine-Konflikt - Macron und Putin - PK
RAis wa Ufaransa Emmanuel Macron akihutubia mkutano wa waandishi habari na rais wa Urusi Vladmir Putin, baada ya mazungumzo yao yaliodumu kwa zaidi ya masaa matano mjini Moscow, Februari 07, 2022.Picha: Thibault Camus/Pool AP/dpa/picture alliance

Mazungumzo ya Macron na Putin siku ya Jumatatu yalidumu kwa zaidi ya masaa matano, na kiongozi huyo wa Ufaransa aliwaambia waandishi habari kwamba hakutarajia Putin kutoa ishara zozote, lakini lengo lake lilikuwa kuzuwia kuongezeka kwa mzozoz huo na kufungua mitazamo mipya, lengo ambalo lilifiwa.

Putin alisema baada ya mkutano huo kuwa Marekani na NATO wamepuuza madai ya serikali yake, lakini aliashiria utayari wake wa kuendelea na majadiliano.

Soma pia: Marekani yatuma wanajeshi, mzozo wa Ukraine ukizorota

Putin alionya kuwa hatua ya kuipatia Ukraine uanachama wa NATO inaweza kusababisha vita kati ya Urusi na muungano huo, endapo Kyiv itachukuwa hatua za kurejesha rasi ya Crimea, ambayo Moscow iliiteka mwaka 2014.

Alisema hatua hiyo itaziburuta nchi za Ulaya katika mzozozo wa kijeshi na Urusi, ambapo hakutakuwa na washindi.

Rais wa Marekani Joe Biden alisema hakuna matarajio ya Ukraine kujiunga na NATO katika muda wa karibuni, lakini yeye na mataifa wanachama wa NATO na NATO yenyewe wanakataa kuondoa uwezekano wa Ukraine kujiunga na muungano huo huko mbeleni.

Soma pia: Wajumbe wa Ukraine na Urusi wakutana Paris

Ukraine-Konflikt - Baerbock
Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock akiwa kwenye uwanja wa mapambano mashariki wa Ukraine, Febrauri 08, 2022.Picha: Bernd von Jutrczenka/dpa/picture alliance

Ziara ya Macron mjini Kyiv, inajiri wakati ambapo waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock, akizuru mkoa wa mashariki mwa Ukraine wa Donbas, ambako amepatiwa maelezo kuhusu hali ya kibinadamu na kijeshi. Serikali ya Ukraine imekuwa katika mzozo wa kivita na waasi wanaotaka kujitenga mashariki mwa taifa hilo tangu mwaka 2014.

Rais Macron anatarajiwa pia kukutana na Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz na rais wa Poland Andrzej Duda mjini Berlin ili kuzingatia sauti za Ulaya Mashariki na misimamo katika kuishughulikia Urusi, kwa sababu huko nyuma, rais huyo wa  Ufaransa ameshthumiwa kuwa karibu sana na Urusi.

Waziri Mkuu wa Romania Vasile Dincu amefahamisha kuwa kundi la kwanza la wanajeshi wa Marekani limewasili nchini humo kuimarisha kikosi cha NATO kwenye ngome yake ya Mashariki.

Dincu amewaambia waandishi habari kuwa wanajeshi 100 wamewasili kushughulikia masuala ya lojistiki.

Chanzo: AFP, AP/DW