1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Lebabon: Zoezi la kuitafuta miili laendelea mjini Beirut

Zainab Aziz Mhariri: Gakuba, Daniel
7 Agosti 2020

Maafisa wa uokoaji bado wanaendelea kuitafuta miili ya watu waliofukiwa kwenye kifusi katika bandari ya Beirut baada ya kutokea mlipuko mkubwa siku tatu zilizopita

https://p.dw.com/p/3gbBB
Libanon Beirut | nach Explosion im Hafenviertel
Picha: Reuters/M. Azakir

Kulingana na mamlaka ya Lebanon miili mingine mitatu imepatikana katika muda wa saa 24 zilizopita. Maafisa wa uokoaji kutoka Ufaransa na Urusi wakisaidiwa na mbwa maalumu wanaendelea na zoezi la kuitafuta miili ya watu pamoja na uchunguzi katika eno la bandari mjini Beirut baada ya Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron kulitembelea eneo palipotokea milipuko hiyo na kuahidi misaada. Macron pia amesema ataendelea kuwasisitizia viongozi wa kisiasa wa Lebanon juu ya mageuzi.

Pamoja na maafisa hao wa uokoaji wadau wa kujitolea wengi pia wamejitokeza kutoka pembe zote za mji mkuu wa Lebanon, Beirut kusaidia katika juhudi kubwa za usafishaji baada ya kutokea mlipuko mnamo siku ya Jumanne. Milipuko mikubwa miwili ilitikisa bandari ya Beirut  na kusababisha vifo vya watu 149 na zaidi ya watu 5,000, wamejeruhiwa.

Moja kati ya majumba yaloyoharibiwa kwenye mlipuko mkubwa mjini Beirut
Moja kati ya majumba yaloyoharibiwa kwenye mlipuko mkubwa mjini BeirutPicha: picture-alliance/Xinhua/B. Jawich

Wakati huo huo Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP linapanga kupeleka nchini Lebanon unga wa ngano kwenye viwanda vya uokaji na nafaka kwenye kampuni za kusaga unga ili kuepuka uhaba wa chakula.

Msemaji wa shirika la WFP ameeleza kwenye mkutano wa Umoja wa Mataifa mjini Geneva amesema WFP ina wasiwasi kwamba uharibifu katika bandari uliosababishwa na mlipuko utazidisha hali mbaya ya usalama wa chakula katika nchi hiyo inayokabiliwa hali mbaya ya kifedha na hasa katika wakati huu wa janga la COVID-19. Msemaji huyo ameeleza kuwa WFP itatoa vifurushi vya chakula kwa maelfu ya familia na pia iko tayari kutoa usimamizi wa ugavi na msaada wa vifaa na utaalam kwa Lebanon.

Vyanzo: AP/RTRE