1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kiongozi wa kijeshi Niger kuunda serikali ya mpito

20 Agosti 2023

Kiongozi wa utawala wa kijeshi uliomuondoa madarakani rais wa Niger aliyechaguliwa kidemokrasia amesena kuwa atairejesha nchi hiyo katika utawala wa kiraia katika miaka mitatu

https://p.dw.com/p/4VMwP
Niger Niamey | Abdourahamane Tiani
Picha: ORTN/Télé Sahel/AFP

Jenerali Abdourahmane Tchiani hakutoa maelezo kuhusu mpango, huo akisema kwenye televisheni ya taifa Jumamosi usiku kuwa kanuni za kipindi cha mpito zitaamuliwa katika siku 30 kupitia mazungumzo yatakayoandaliwa na utawala huo wa kijeshi.

Soma pia: Maafisa wa Mali, Burkina Faso na Niger wakutana Niamey

Ghana Accra | ECOWAS Treffen
Wakuu wa kijeshi wa ECOWAS walikutana GhanaPicha: Richard Eshun Nanaresh/AP Photo/picture alliance

"Nna uhakika kuwa…..tutafanya kazi kwa Pamoja ili kupata ufumbuzi wa mzozo huu, katika maslahi ya wote,” alisema Tchiani, akizungumza baada ya mkutano wake wa kwanza na ujumbe wa kikanda unaoongoza juhudi za kuutatua mgogoro wa taifa hilo la Afrika Magharibi.

"Dhamira yetu sio kukamata madaraka," aliongeza: "Kama shambulizi litafanywa dhidi yetu, haitakuwa kazi rahisi kama wanavyodhani baadhi ya watu.”

Soma pia: ECOWAS yasema jeshi lipo tayari kuingia Niger

Ujumbe wa ECOWAS, ukiongozwa na rais wa zamani wa Nigeria Jenerali Abdulsalami Abubakar, pia ulikutana katika kikao tofauti na Rais aliyepinduliwa Mohamed Bazoum. Ulijiunga na juhudi za maridhiano zinazoendeshwa na Leonardo Santos Simao, mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa katika eneo la Afrika Magharibi na Sahel, aliyewasili Ijumaa.

ECOWAS mnamo Agosti 10 iliamuru kupelekwa kwa jeshi la Pamoja kwa ajili ya kurejesha utawala wa kikatiba nchini Niger. Kamishna wa ECOWAS anasehusika na masuala ya amani na usalama Abdel-Fatau Musah, amesema Ijumaa kuwa nchi 11 kati ya 15 wanachama zimekubaliana kuchangia askari kwenye jeshi hilo la uingiliaji akisema wako tayari Kwenda.

Ufafanuzi:Kwanini Niger ni muhimu kwa mataifa ya magharibi?

Soma pia: Umoja wa Ulaya kuichukulia hatua kali Niger

Nchi wanachama waliokubali kuingilia Niger kijeshi hawakujumuisha nchi tatu za jumuiya hiyo zilizo chini ya utawala wa kijeshi kufuatia mapinduzi: Guinea, Mali na Burkina Faso.

Siku ya Ijumaa, televisheni ya taifa ya Niger ilisema Mali na Burkina Faso zimepeleka ndege za kivita kuonyesha mshikamano.

Kwenye mita ya Niamey Jumamosi, wakaazi wengi walisema wamejiandaa kupambana dhidi ya uingiliaji wa jeshi la ECOWAS. Maelfu ya watu walijitokeza nje ya uwanja mkuu wa michezo kujisajili kama wapiganaji na watu wa kujitolea kusaidia na mahitaji mengine kama utawala wa kijeshi utahitaji msaada. Baadhi ya wazazi waliwapeleka Watoto wao kujisajili.

ap, afp, reuters, dpa