1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Polisi Kenya yapiga marufuku maandamano Nairobi

Angela Mdungu
18 Julai 2024

Jeshi la polisi nchini Kenya limepiga marufuku maandamano kufanyika jijini Nairobi hadi itakapotangazwa tena. Jeshi hilo limechukua hatua hiyo kwa sababu makundi ya wahalifu sasa yamejiingiza kwenye maandamano hayo

https://p.dw.com/p/4iSXb
Kenia | Proteste gegen den kenianischen Präsidenten William Ruto in Nairobi
Picha: TONY KARUMBA/AFP/Getty Images

Kauli ya polisi ya kuyapiga marufuku maandamano katikati mwa jiji la Nairobi imetolewa baada ya wiki kadhaa za maandamano ya kuipinga serikali.

Mkuu wa polisi, Kanja Kiricho alisema katika taarifa aliyoitoa Jumatano jioni kuwa jeshi la polisi limepata taarifa za kuaminika za kiitelijensia kuwa, makundi ya uhalifu wa kupangwa yanapanga kuyatumia maandamano yanayoendelea ili kufanya mashambulizi yakiwa ni pamoja na uporaji.

Ameongeza kuwa maandamano hayo pia yamepigwa marufuku katika maeneo yanayozunguka eneo la biashara jijini Nairobi ili kuhakikisha usalama wa umma.

Soma zaidi: IGP Kenya ajiwajibisha kwa vifo vya waandamanaji

Awali, wanaharakati walitoa wito kwa watu kukusanyika  Alhamisi katika viwanja vya Uhuru huku polisi wakitanda katikati mwa Nairobi. Wanaharakati hao wanasema kuwa wanataka Rais Ruto aachie ngazi. Pia, wametoa wito wa kutaka  mageuzi ili kushughulikia ubadhirifu, na  utawala mbovu.

Watu wasiopungua 50 wameuwawa tangu yalipoanza maandamano yanayoongozwa na vijana mwezi mmoja uliopita. Maandamano hayo yalianza kwa kwa kupinga muswada tata wa fedha uliotoa mapendekezo ya kuongeza ushuru lakini yaliendelea licha ya Rais William Ruto kuuondoa na kulivunja baraza la mawaziri.

Mgogoro mkubwa tangu Rais Ruto aingie madarakani

Maandamano hayo yaliyoratibiwa kwa njia ya mtandao bila ya uungwaji mkono kutoka kwa wanasiasa wa vyama vya upinzani, yametengeneza mgogoro mkubwa zaidi katika miaka miwili wa rais Ruto madarakani. Yalianza kwa amani  lakini baadaye yalikumbwa na vurugu.

Rais William Ruto anakabiliwa na maandamano ya kumtaka aondoke madarakani
Rais wa Kenya, William RutoPicha: Brendan Smialowski/AFP/Getty Images

Wiki iliyopita, Rais William Ruto, aliahidi kuunda serikali ya kitaifa lakini muungano wa vyama vya upinzani ulikataa wazo hilo na badala yake unataka utawala unaofuata katiba.

Soma zaid: Shinikizo zaiandama serikali ya Kenya kuwatuliza waandamanaji

Ofisi yake, ilipanga kufanya mazungumzo na sekta mbalimbali wiki hii ili kuyashughulikia manung'uniko ya waandamanaji  lakini hadi kufikia Alhamisi, hakukuwa na dalili ya kuanza kwa majadiliano hayo. Wengi wa viongozi wa maandamano wamekataa mwaliko wa ofisi ya Rais Ruto na badala yake wanataka masuala kama rushwa yashughulikiwe haraka.

Katika hatua nyingine, mamlaka ya mawasiliano ya Kenya imevitahadharisha vyombo vya habari dhidi ya kuchochea vurugu katika matangazo yao yanayohusu maandamano. Mamlaka hiyo kupitia Mkuu wake David Mugonyi imesema kufanya hivyo kunaweza kusababisha machafuko ndani ya taifa hilo.