1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yazishambulia Palestina, Syria

22 Oktoba 2023

Ndege za kivita za Israel zimeyashambulia maeneo kadhaa mjini Gaza pamoja na viwanja viwili vya ndege nchini Syria na pia msikiti mmoja katika eneo la Ukingo wa Magharibi unaodaiwa kutumiwa na wanamgambo wa Hamas.

https://p.dw.com/p/4Xrzj
Wapalestina wakiangalia sehemu ya madhara ya mashambulizi ya Israel kwenye kiunga cha Rafah kusini mwa Gaza siku ya Jumapili, 22 Oktoba 2023.
Wapalestina wakiangalia sehemu ya madhara ya mashambulizi ya Israel kwenye kiunga cha Rafah kusini mwa Gaza siku ya Jumapili, 22 Oktoba 2023.Picha: Said Khatib/AFP

Mashambulizi hayo ya usiku wa kuamkia Jumapili (Oktoba 22) yalifanyika wakati malori yaliyosheheni misaada ya kibinaadamu yakianza kuingia katika eneo lililozingirwa la Gaza. 

Msemaji wa jeshi la Israel alisema nchi hiyo inaongeza mashambulizi yake ya anga na kuna matarajio pia ya vikosi vya ardhini kuanzisha mashambulizi katika eneo hilo.

Soma zaidi: Israel yaionya Hizbullah kuiingiza Lebanon vitani

Vita hivyo vilivyoingia siku yake ya 16 vinatajwa kuwa vita vikali zaidi kwa pande zote mbili, kati ya vita vitano vilivyowahi kushuhudiwa katika ukanda huo baina ya Israel na kundi la Hamas.

Kulingana na wizara ya afya ya Gaza, watu 4,385, wameuwawa hadi sasa huku wengine 13,561 wakijeruhiwa. 

Soma zaidi: Maelfu ya waandamanaji wanayoiunga mkono Palestina waandamana katika miji mbali mbali duniani

Israel imesema inaamini watu 212 wamechukuliwa mateka na wanamgambo wa Hamas wakati walipofanya mashambulizi yake dhidi ya taifa hilo Oktoba Saba na kuwaua zaidi ya watu 1,400.