1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hamas yakataa pendekezo la kusitisha mapigano kwa muda

26 Desemba 2023

Kundi la wanamgambo wa Hamas limekataa pendekezo la kusitisha mapigano kwa muda na Israel badala yake kutoa wito wa kusitishwa mapigano, ili kurudisha amani ya kudumu.

https://p.dw.com/p/4aa6i
Gaza / Uharibifu baada ya mashambulizi ya anga ya Israel kwenye kambi ya wakimbizi ya Al-Maghazi
Wapalestina wakikagua uharibifu katika kambi ya wakimbizi ya Al-Maghazi baada ya shambulio la usiku la Israel mnamo Desemba 25, 2023, huku kukiwa na mapigano yanayoendelea kati ya Israel na kundi la wanamgambo la Hamas. Picha: Mahmud Hams/AFP

Hamas wametoa kauli hiyo baada ya ripoti kuwa Misri imependekeza njia za kuumaliza mzozo kati ya Israel na Hamas kwa mpango kabambe wa kusitisha mapigano.

Soma pia: Hamas, Islamic Jihad wakataa pendekezo la Misri kuachia madaraka Gaza

Kwa mujibu wa vyombo vya habari na wanadiplomasia, pendekezo la Misri la kumaliza vita katika Ukanda wa Gaza lingefanyika katika awamu kadhaa,  ya kwanza ikiwa ni kusitisha mapigano kwa angalau siku 14 halafu mateka 40 wa Israel wanaoshikiliwa huko Gaza wataachiwa kwa kubadilishana na Wapalestina 120 walio jela nchini Israel na hatimaye, Israel kuyaondoa majeshi yake kutoka kwenye ardhi ya Palestina.

Soma pia: Mashambulizi ya Israel yaua 100 katika mmoja ya usiku mbaya zaidi wa vita Gaza

Wakati huo huo msimaizi wa kundi la watoa misaada wa Umoja wa Mataifa, Gemma Connell amenukuliwa na shirika la habari la Reuters akisema watu waliokimbia makazi yao katika Ukanda wa Gaza wanahangaika kupata maeneo ya kuhamia.

Kulingana na takwimu za Umoja wa Mataifa, takriban wakazi milioni 1.9 kati ya wakazi zaidi ya milioni 2.2 wa Gaza wameyakimbia makazi yao kutokana na mapigano. Zaidi ya asilimia 40 ya makazi katika eneo la Gaza yameharibiwa.