1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Corona: Idadi ya vifo yapindukia watu 800 nchini China

Zainab Aziz Mhariri: Sudi Mnette
9 Februari 2020

Idadi ya watu waliokufa kutokana na maambukizi ya virusi vya corona nchini China imeongezeka kwa vifo 89 na kufikia watu 811. Mmarekani na Mjapani ni raia wa kwanza wa kigeni kufa tangu kuzuka kwa mripuko huo.

https://p.dw.com/p/3XTuD
China Coronavirus l  Notfall-Krankenhaus in Wuhan - erste Patienten werden verlegt
Picha: picture alliance/Xinhua/X. Yijiu

Idadi hiyo ya watu waliokufa kutokana na maambukizi ya virusi vya corona sasa imepindukia idadi ya waliokufa kutokana na ugonjwa wa homa ya SARS mnamo mwaka 2002 na 2003 nchini China. Jumla ya watu 800 walikufa duniani kote. Shirika la afya duniani WHO limesema hadi sasa kuna jumla ya maambukizi 34,800 duniani kote. China bara ndio iliyoathirika zaidi mpaka sasa imethibitishwa kwamba watu 27,000 wameambukizwa.

Ubalozi wa Marekani ulitoa taarifa Jumamosi kuhusu raia wake mwenye umri wa miaka 60 aliyefariki baada ya kuambukizwa virusi vya corona. Waliokufa wengi wanatoka katika mkoa wa kati wa Hubei, ambako virusi vya corona viligunduliwa kwa mara ya kwanza.

Wuhan: Wagonjwa wakiwasili kwenye hospitali mpya ya Leishenshan
Wuhan: Wagonjwa wakiwasili kwenye hospitali mpya ya LeishenshanPicha: picture-alliance/Photoshot

Raia watano wa Uingereza akiwemo mtoto wamegundulika kuwa na virusi hivyo nchini Ufaransa. Waziri wa Afya wa Ufaransa Agnes Buzyn amesema raia hayo waliambukizwa na raia mwingine wa Uingereza ambae katika siku za hivi karibuni alikuwa nchini Singapore.

Hospitali ya dharura ya pili imekamilika na imefunguliwa katika jiji la Wuhan, linalokabiliana na mlipuko wa virusi vya  corona. Hospitali hiyo kwa jina Leishenshan ina wodi za kulaza wagonjwa 32 na jumla ya vitanda 1,500 pamoja na chumba kimoja cha upasuaji. Kikosi cha kwanza cha madaktari kilifika siku ya Jumamosi asubuhi.

Jiji la Wuhan linabadilika kwa haraka wakati ambapo majengo kadhaa yanageuzwa kuwa hospitali ili kukabiliana na idadi kubwa ya watu walioambukizwa virusi vya corona. Hospitali nyingine iliyojengwa kwa muda mfupi yenye vitanda 1,000 ilifunguliwa siku ya Jumatatu. Ujenzi wake ulichukua siku 10. Kufikia Jumamosi, mkoa wa kati wa Hubei pekee uliorodhesha idadi ya watu 27,100 waliokuwa wameambukizwa virusi vya corona, watu 780 wameaga dunia kwenye mkoa huo.

Chanzo:/AFP/https://p.dw.com/p/3XSJr