1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chanjo mpya ya Ebola kuanza kutumika Congo

21 Septemba 2019

Mamlaka za afya Kongo zapanga kuanza kutumia chanjo mpya ya Ebola inayozusha utata miongoni mwa maafisa wa afya nchini humo zikiweko hisia chanjo hiyo huenda sio salama na haina ufanisi

https://p.dw.com/p/3Q0K0
Kongo Ebola Ausbruch
Picha: Reuters/J. Akena

Maafisa wa afya katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo wamesema wanapanga kuanza kuitumia chanjo ya pili ya Ebola iliyotengenezwa na kampuni ya Johnson&Johnson,ili kukabiliana na mripuko wa ugonjwa huo.

Timu inayofuatilia mapambano dhidi ya maradhi hayo nchini Kongo haijasema lini haswa chanjo hiyo itaanza kutumika. Chanjo hiyo itatumika kuchukuwa nafasi ya chanjo nyingine ya Ebola iliyotengenezwa na kampuni ya Merck iliyotumiwa kwa watu zaidi ya 225,000 tangu mwezi Agosti mwaka 2018.

Chanjo ya J&J imekuwa chanzo cha utata miongoni mwa maafisa wa afya nchini Kongo. Aliyekuwa waziri wa afya aliyefutwa kazi kutokana na sakata la madai ya kusimamia vibaya mapambano dhidi ya Ebola mwezi Julai anapinga matumizi ya chanjo hiyo akisema bado haijathibitishwa  kuwa salama au kuwa na ufanisi.

Kongo Ebola Ausbruch
Picha: Reuters/O. Acland

Lakini kwenye taarifa yake, timu ya sasa ya kukabiliana na Ebola imesema chanjo hiyo ni  salama na kugusia kwamba tayari imeshafanyiwa majaribio katika nchi jirani ya Uganda na Guinea huko Afrika Magharibi. Timu hiyo imehoji  kwamba ni kwa nini chanjo iliyokwisha tumiwa na nchi jirani kwanini Congo isitumike kuulinda umma wake?

Katika taarifa hiyo maafisa wa afya wanalenga kuanza kuitowa chanjo hiyo ya J&J kwa wakongomani wafanyabiashara wanaovuka mpaka kuingia nchi za Rwanda pamoja na wakaazi wa mikoa inayopakana na kitovu cha mripuko huo ili kujenga mfumo wa kupambana na maradhi hayo miongoni mwa watu wa eneo hilo.

Mripuko huu mpya wa Ebola umeshaua zaidi ya watu 2,100 tangu katikati ya mwaka uliopita,ukiwa ni mripuko wa pili kwa ukubwa baada ya ule ulioshuhudiwa mwaka 2013 mpaka 2016 katika nchi za Afrika Magharibi ambapo watu 11,300 walifariki.

Mwandishi: Saumu Yusuf

Mhariri: Angela Mdungu

 

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW