1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chadema: Tutatumia mbinu binafsi kulinda kura zetu

George Njogopa/DW Dar es Salaam25 Juni 2020

Chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania, Chadema kimesema kitatumia mbinu binafsi kulinda kura zake katika uchaguzi mkuu ujao kutokana na kutoiamini tume ya taifa ya uchaguzi iliyopo.

https://p.dw.com/p/3eKbH
Die Vorsitzende des CHADEMA-Frauenflügels Halima Mdee
Picha: DW/E. Boniphace

Chama hicho ambacho kimedai kina matarajio ya kufanya vizuri katika matokeo ya uchaguzi wa mwezi Oktoba kimesema hakina chaguo lingine mbali ya kuwa na mbinu mbadala ya kusimamia kura zake.

Kimedai hatua hiyo inatokana na kutoiamini tume ya uchaguzi iliyopo baada ya kilio chao cha miaka mingi kutopatiwa ufumbuzi.

Katibu mkuu wa chama hicho, John Mnyika ambaye leo amekutana na waandishi wa habari hata hivyo hakubainisha moja kwa moja jinsi watavyoutekeleza mkakati huo.

11 wawania kuipeperusha bendera ya Chadema

Suala hilo la wapinzani kulinda kura zao ilikuwa mada iliyozua mvutano mkubwa wakati wa uchaguzi mkuu uliopita wa 2015. Nalo suala la tume huru imekuwa ajenda ya kipekee kwa vyama vya upinzani ambavyo mara zote vimekuwa vikiikosoa tume iliyopo kwa madai kuwa haitoi uwakilishi kwa washiriki wote wa uchaguzi.

Viongozi wa Chadema wameshikilia msimamo wao kuwa shambulizi dhidi ya mwenyekiti wao Freeman Mbowe lilichochewa kisiasa
Viongozi wa Chadema wameshikilia msimamo wao kuwa shambulizi dhidi ya mwenyekiti wao Freeman Mbowe lilichochewa kisiasaPicha: DW/E. Boniphace

Wakataziri wa zamani wa mambo ya Nje, Bernard Membe ambaye amezua mjadala mkubwa kutokana na kauli yake ya kutaka kuwania urais wa mwaka huu, ameingia katika ajenda hiyo akisisitiza pia haja ya kuwa na tume huru. Hata hivyo, serikali imekuwa ikidai kuwa tume iliyopo ni huru na imeundwa kwa mujibu wa katiba na sheria.

Chadema: Shambulizi dhidi ya Mbowe lilichochewa kisiasa

Ama kwa upande mwingine, Chadema imesisitiza tena kuwa mwenyekiti wake, Freeman Mbowe alishambuliwa kisiasa huku kikipuuza taarifa zinazotolewa kwamba kiongozi huyo hakufanyiwa shambulio lolote zaidi ya kukutwa akiwa amepata kilevi.

Chama hicho kimelitupia lawama jeshi la polisi kwa madai kwamba linajaribu kipindisha ukweli wa mambo kuhusiana na tukio hilo, lililotokea wakati wa vikao vya bunge vikiendelea.

Mbali na hilo, chama hicho ambacho hivi karibuni kilitangaza majina ya wagombea 11 waliojitokeza kuwania nafasi ya urais, kimedai kuwepo kwa viashiria kwamba jeshi hilo la polisi linajitumbukiza katika masuala ya kisiasa na hivyo kufanya uwanja wa kisiasa kushindwa kutoa uwiano sawa kwa washiriki wa uchaguzi mkuu kuchuana kwa hoja na sera.