1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chad: mwaka mmoja baada ya kifo cha Déby

Hawa Bihoga
20 Aprili 2022

Utawala wa kijeshi wa Chad bado haujafanya maendeleo makubwa katika kuirejesha nchi kwenye utawala wa kiraia tangu jeshi kutwaa mamalaka baada ya kifo cha kiongozi wa zamani wa taifa hilo Idriss Déby mwaka jana.

https://p.dw.com/p/4A8it
Tschad l Mahamat Idriss Deby , Militär
Picha: Christopeh Petit Tesson/AFP/Getty Images

Hii leo umetimia mwaka mmoja kamili tangu aliyekuwa kiongozi wa muda mrefu wa Chad, Idris Deby Itno, kufariki ghafla akiwa katika uwanja wa mapambano dhidi ya waasi wa kundi  linalojiita FACT.

 Mtoto wa Deby, Jenerali Mahamat Idriss Deby, alichukuwa madaraka mara moja kwa msaada wa jeshi, kwa hoja kuwa angeliendeleza urathi wa baba yake aliyekaa madarakani kwa miaka 30.

Lakini mwaka mmoja baadaye, utawalawake wa kijeshi umepiga hatua ndogo sana katika kurejesha amani na demokrasia nchini humo.

Kwa muda mrefu, mataifa ya Magharibi yalimchukilia Dedy kama mtawala mwenye nguvu aliyejitolea kupambana dhidi ya magaidi wanaoendesha shughuli zao ndani ya kanda ya Sahel na hivyo, hatua ya mwanawe kuchukua madaraka ilionekana kama uhakikisho wa kuendeleza mapambano hayo.

Soma zaidi:UN yaelezea hofu juu ya vurugu katika kanda ya Sahel

Serikali ya sasa ya mpito inayoongozwa na Jenerali Deby ilikuwa imeahidi mwaka jana kwamba jeshi lingelifanya uchaguzi wa kidemokrasia ndani ya kipindi cha miezi 18.

Hata hivyo, muda huo unakaribia kuisha na wachambuzi wengi wanaelezea hofu kwamba mazingira ya uchaguzi hayapo.

Wachambuzi: Hakuna mabadiliko makubwa hadi sasa

Mchambuzi wa masuala ya ulinzi kutoka kituo cha usalama wa raia na ujenzi wa amani, Adib Saani, aliiambia DW kwa njia ya simu kutokea mji mkuu wa Ghana, Accra, kwamba hakuna kubwa lililobadilika tangu Jenerali Mahamati Deby alipochukuwa madaraka:

"Bado wanapaswa kushughulika na masuala ya uasi, na ukosefu wa usalama ni tatizo kubwa Sahel"

Alisema Saan katika mazungumzo yake na Dw kwa njia ya simu.

Wakati Jenerali Deby alipotangaza mipango ya kutawala na baraza la kijeshi la wajumbe 15 mnamo mwezi Aprili mwaka jana, haikuchukuwa muda mrefu kabla ya mizozo kuibuka.

Utawala wa kijeshi wataka mazungumzo na waasi

N'Djamena, Chad | Demonstration gegen die Junta
Wachad wakiandamana kupinga utawala wa kijeshi uliochukua hatamu tangu kifo cha kiongozi wao Deby ItnoPicha: Djimet Wiche/AFP/Getty Images

Mwaka mmoja baadaye, utawala wa kijeshi unapambana kufikia makubaliano na waasi, ambao matendo yao yalipekea kifo cha baba yake.

Mazungumzo na makundi ya waasi yanayofanyika mji mkuu wa Qatar, Doha, yaliyoanza Machi 13 kufuatia ucheleweshaji, hayajakuwa na ufanisi mkubwa.

Waasi wa Chad na wajumbe wa utawala wa kijeshi wamekuwa wakikataa kukutana ana kwa ana kwenye meza ya mazungumzo muda wote.

Soma zaidi:machafuko Sahel yachangia njaa kwa mamilioni ya watu

Licha ya hayo, utawala wa kijeshi ulisema unatumaini kuitisha mkutano wa kitaifa kufikia Mei 10 ambao utaidhinisha mpango wa kurejea kwenye utawala wa kiraia.

Mazungumzo hayo ya kitaifa yalinuwiwa kuvishirikisha vyama mbalimbali na makundi yenye silaha kutoka kote nchini.

Waasi waonesha wasiwasi dhidi ya utawala wa kijeshi

Mipango hiyo sasa inakabiliwa na kitisho, ambapo waasi walio na mashaka bado na utawala wa kijeshi na upinzani wa kisiasa wa Chad, wanatishia kuususia mkutano huo, jambo ambalo linazidisha ugumu wa hali nchini humo.

Afrika Tschad Konflikt  Armee Soldaten gegen Rebellen in Ziguey
jeshi la Chad katika oparesheni ya kijeshi kukabiliana na waasi wa FACTPicha: Abdoulaye Adoum Mahamat/AA/picture alliance

Saani alisema hakuwezi kuwepo na suluhisho la kudumu kwa mzozo nchini Chad au hata kurejesha utawala wa kiraia hadi pale makundi ya upinzani yanayohusika, yatakapokuwa tayari kuafikiana.

Jumuiya ya kimataifa ikiongozwa na Ufaransa, ilikuwa imeonyesha uungaji mkono kwa Mahamat Idriss Deby Itno kufuatia kifo cha baba yake, licha ya hapo awali kuonyesha upinzani dhidi ya muelekeo ya mapinduzi ya kijeshi barani Afrika. Jenerali Deby alipata hata kuidhinishwa na Umoja wa Ulaya.

Soma zaidi:Chad yataja serikali mpya ya mpito

Saani anasema licha ya Umoja wa Ulaya kutamani kuendeleza mapambano dhidi ya uasi wa makundi ya itikadi kali katika ukanda huo, utataka kuona dhamira zaidi kuelekea mchakato wa mpito kwa upande wa utawala wa kijeshi.