1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Biden akutana na viongozi wa NATO wa mashariki mwa Ulaya

23 Februari 2023

Rais wa Marekani Joe Biden amekutana na viongozi wa nchi za upande wa mashariki mwa Ulaya, ambao ni wanachama wa jumuiya ya Kujihami ya NATO.

https://p.dw.com/p/4Nrke
Warschau NATO-Treffen Bukarest 9
Picha: MANDEL NGAN/AFP

Kwenye mkutano huo wa Jumatano huko Warsaw Poland, Biden alikariri kujitolea kwa nchi yake kuhakikisha usalama wa washirika wake wa mashariki mwa Ulaya. Kauli yake imejiri baada ya Urusi kujitoa katika mkataba kati yake na Marekani wa kudhibiti silaha za nyuklia. Biden alitaja hatua hiyo ya Urusi kujiondoa kwenye makubaliano hayo kuwa kosa kubwa.

Alisisitiza kuhusu kifungu cha 5 cha jumuiya ya NATO kinachoelezea mkakati wa pamoja wa ulinzi wa jumuiya hiyo.

Mkutano huo uliwaleta pamoja wakuu wa nchi tisa maarufu kama Bucharest Tisa, ambazo ni Bulgaria, Jamhuri ya Czech, Estonia, Hungary, Latvia, Lithuania, Poland, Romania na Slovakia.

Biden aliwaambia kuwa "Kama wanachama wa NATO mlioko mashariki mwa Ulaya, mko mstari w ambele wa ulinzi wetu wa pamoja. Na mnajua kuliko yeyote yule kile kilichoko hatarini kwenye mzozo huu. sio tu Ukraine bali pia uhuru wa demokrasia kote Ulaya na ulimwenguni."

Rais Biden asema NATO ndio muungano imara zaidi

Rais wa Lithuania Gitanas Nauseda amesema alimtaka Biden kutumia zana za ziada za kijeshi zilizoko katika mataifa ya Baltic.

Nchi za 'Bucharest Tisa' zimekuwa zikiunga mkono kwa dhati juhudi za misaada ya kijeshi kwa Ukraine, na zimetoa wito wa misaada zaidi kama mifumo ya ulinzi ya angani kwa taifa hilo linalozongwa na vita.
Nchi za 'Bucharest Tisa' zimekuwa zikiunga mkono kwa dhati juhudi za misaada ya kijeshi kwa Ukraine, na zimetoa wito wa misaada zaidi kama mifumo ya ulinzi ya angani kwa taifa hilo linalozongwa na vita.Picha: EVELYN HOCKSTEIN/REUTERS

Rais wa Romania Klaus Lohannis alisema nchi za Magharibi zinapaswa kushirikiana katika kuisaidia Ukraine hadi mzozo huo utakapomalizika na ivishine vita hivyo.

Si wanachama wote wa kundi la Bucharest Tisa wamekuwa tayari kuisaidia Ukraine mfano Hungary ambayo imepuka ikipinga baadhi ya vikwazo vya Umoja wa Ulaya kwa Urusi.

Biden afanya ziara ya kustukiza Kyiv kuelekea mwaka mmoja wa uvamizi

Pamoja na Uturuki, Hungary haijaridhia maombi ya Sweden na Finland kuwa wanachama wa NATO.

Mnamo wakati kuna mvutano mkubwa zaidi kati ya Urusi na nchi za Magharibi Kuwahi shuhudiwa tangu enzi za vita Baridi miongo mitatu iliyopita, Biden aliwahutubia maelfu ya watu mjini Warsaw siku ya Jumanne ambapo alisema watawala wa kimabavu kama rais wa Urusi Vladimir Putin sharti wapingwe.

Urusi imekuwa ikisema inatizama jumuiya ya NATO kitisho kwake kiusalama.

(Chanzo: RTRE)