1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BERLIN: Nchi za Asia zakosolewa kwa ukiukaji wa haki za binadamu

28 Mei 2007
https://p.dw.com/p/CBxH

Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International tawi la Ujerumani limezishutumu nchi kadhaa za Asia kwa visa mbalimbali vya ukiukaji wa haki za binadamu.

Shutuma hizo zimetolewa huku ukikaribia kufanyika mkutano wa mawaziri wa mashauri ya kigeni kutoka Asia na Ulaya mjini Hamburg hapa Ujerumani.

Wajumbe wa shirika la Amnesty International wanaokutana mjini Munich hapa Ujerumani wamesema hukumu ya kifo inaendelea kutumiwa sana katika mataifa ya Asia na serikali zao zimevitumia vita dhidi ya ugaidi vinavyoongozwa na Marekani kuukandamiza upinzani.

Shirika hilo pia limeyakosoa mataifa ya Umoja wa Ulaya kwa ukiukaji wa haki za binadamu kwa kufanya biashara na China na Urusi. Mkutano huo wa siku mbili wa mawaziri wa mashauri ya kigeni mjini Hamburg unatarajiwa kutuwama juu ya mizozo ya nyuklia ya Korea Kaskazini na Iran.

Sambamba na hayo, maelfu ya waandamanaji wameandamana katika barabara za mjini Hamburg kuupinga mkutano huo na juhudi za polisi kuzuia maandamano kabla kufanyika mkutano wa kilele wa nchi za G8 katika mji wa mapumziko wa Heiligendamm hapa Ujerumani.