1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Baerbock: Urusi inaendelea kutengwa na Jumuiya ya Kimataifa

Angela Mdungu
22 Septemba 2023

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani, Annalena Baerbock amesema Urusi inaendelea kutengwa na Jumuiya ya kimataifa kutokana na vita vyake dhidi ya Ukraine.

https://p.dw.com/p/4WgkT
Annalena Baerbock
Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani, Annalena Baerbock(katikati)Picha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Annalena Baerbock, Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani jana Alhamisi aliliambia shirika la habari la DPA kuwa Urusi ilikosolewa wazi kwa kukiuka kwake azimio la Umoja wa Mataifa wakati wa mkutano wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa na katika Baraza la Usalama la umoja huo. Ni wakati taifa hilo likiendelea kutengwa kutokana na uvamizi wake dhidi ya taifa jirani la Ukraine.

Baerbock aliongeza kuwa Moscow illikabiliwa na upinzani mkali zaidi ilipojaribu kuhoji umuhimu wa maazimio muhimu kuhusu maendeleo endelevu na afya hasa kuhusu mataifa ya Africa, Amerika ya Kati na nchi za bara la Asia. 

Soma pia: Zelensky na Lavrov watarajiwa kuhudhuria Mkutano wa Baraza Kuu la UN

Katika hatua nyingine, kiongozi wa mamlaka ya Palestina, Mahmud Abbas ameuambia Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuwa,  amani haiwezi kupatikana Mashariki ya Kati bila suluhisho la kuwepo kwa mataifa mawili. Kauli hiyo ni ya tahadhari kwa Saudi Arabia ambayo inatafakari kuitambua Israel.

Mahmud Abbas
Kiongozi wa mamlaka ya Palestina, Mahmud AbbasPicha: Palestinian Presidency /Handout/AA/picture alliance

Naye kiongozi pekee wa kijeshi aliyehudhuria mkutano huo kutoka barani Afrika, Kanali Mamady Doumbuya wa Guinea, ametetea hatua ya majeshi kuingilia masuala ya kisiasa kutokana na mfululizo wa mapinduzi ya kijeshi barani Afrika.

Akizungumza katika mkutano huo, Kanali Doumbouya amesema; "ni wakati muafaka wa kuzitambua haki zetu, kuhakikisha tunakuwa tunakostahili, zaidi ya hayo, ni wakati sasa wa kuacha kutufundisha, kutupelekesha na kutufanya kama watoto."

Hotuba ya viongozi wa afrika katika mkutano wa UNGA; Viongozi hao kadhaa wa Afrika wahutubia kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa akiwemo Rais wa Jamhuri ya Afrika ya Kati Faustin Archange Toudera

Tukisalia katika mkutano huo China iliwaambia viongozi wa dunia waliohudhuria kuwa, inajiona kama sehemu ya mataifa yenye maendeleo duni. Makamu wa Rais Han Zheng aliyemuwakilisha Rais Xi Jin Ping amebainisha kuwa China inazielewa changamoto zilizo kwenye nchi ambazo hazina maendeleo na inataka kuzipa mbadala wa kile ilichokiita "kuongozwa na mataifa ya magharibi":