1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUkraine

Baerbock: Tutapeleka misaada zaidi Ukraine bila kuyumba

Hawa Bihoga
11 Septemba 2023

Waziri wa Mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock amefanya ziara ya kushtukiza mjini Kiev leo, akiahidi uungwaji mkono usiyoyumba kwa Ukraine na kusifu maendeleo yake kuelekea uanachama wa Umoja wa Ulaya.

https://p.dw.com/p/4WBuA
Polen Medyka | Annalena Baerbock reist nach Kiew
Annalena Baerbock akiwa ziarani kievPicha: Dominik Butzmann/Imago Images

Katika taarifa iliyotolewa na wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani, Waziri Baerbock alisifu ujasiri na dhamiri ya Ukrainekulinda uhuru wa watu wote wa Ulaya, na kusisitiza kwamba nchi hiyo inaweza kuitegemea Ujerumani kama shukrani.

Alisema Ujerumani haitutapunguza juhudi zake kuisadia Ukraine katika harakati za kujilinda dhidi ya uvamizi wa Urusi.

"Tutatuma misaada ya kiuchumi, Kijeshi na katika nyanja ya kiutu," alisema Baerbock.

Hii ni ziara ya nne ya waziri huyo nchini Ukraine tangu kuanza kwa uvamizi wa Urusi mnamo Febrauri 2022.

Juhudi za Ukraine kujiunga na Umoja wa Ulaya zinatarajiwa kuwa miongoni mwa mada za majadiliano na maafisa wa Ukraine wakati wa ziara hiyo.

Ukraine ilipatiwa hadhi ya nchi mgombea wa uwanachama wa Umoja wa Ulaya mwaka mmoja uliopita na ina matumaini ya kuanza mazungumzo rasmi mwaka huu juu ya nini inahitaji kufanya kuimarisha mambo yake.

Baerbock amesema Ukraine tayari imepiga hatua nzuri katika baadhi ya maeneo ikiwemo mageuzi ya sheria, lakini bado ina safari kidogo katika kukabiliana na rushwa.

Amerejelea msaada usioyumba kwa Ukraine katika njia yake ya kuwa mwanachama wa Umoja wa Ulaya.

Katika taarifa hiyo, Baerbock pia alionyesha kusikitishwa na kulazimishwa kwa uhamisho wa watoto wa Ukraine kwenda Urusi, na kusema Rais Putin atafanya kila kitu kuwavunja watu wa Ukraine.

Ukraine yathibitisha kukomboa maeneo zaidi

Ukraine imesema leo kuwa vikosi vyake vimefanikiwa kurejesha maeneo kadhaa kusini na mashariki mwa nchi, na kupigana hadi kijiji kimoja katika mkoa wa Donetsk wiki iliyopita.

Ukraine | Krieg | Panzerabwehrraketensystem Stugna
Askari akiwa katika uwanja wa mapambano huko BakhmutPicha: Roman Chop/AP Photo/picture alliance

Naibu waziri wa ulinzi Ganna Malyar amesema vikosi vya Ukraine vimesonga mbele karibu na mji wa Bakhmut, mashariki mwa nchi, ambao ulitekwa na Urusi mwezi Mei.
Alisema katika wiki iliyopita, kilomita za mraba mbili zimekombolewa katika eneo la Bakhmut, na jumla ya kilomita za mraba 49 zimekombolewa karibu na Bakhmut.

"Vikosi vyetu vinapiga hatua katika eneo la Opytne, na tayari vimechukua sehemu ya eneo hilo."

Aliongeza kwamba kuna mafanikio kidogo katika eneo la Novamaiorske.

"Kwa kweli, vikosi vya kijeshi vya Ukraine sasa vinaimarisha nafasi yake huko.''

Ukraine imepeleka sehemu kubwa ya rasilimali zakekupigana kwenye eneo la kusini, ambapo jeshi limevunja safu ya kwanza ya ulinzi ya Urusi na kuteka vijiji kadhaa.

Jeshi la Ukraine limeripoti pia hii leo kwamba vikosi vyake vimekomboa maeneo kadhaa ya visima vya mafuta karibu na Rasi ya Crimea, kupitia kila idara ya intelijensia ya jeshi imesema ni operesheni ya kipekee.

Kiev yapuuza uchaguzi mdogo wa Urusi

Tume kuu ya uchaguzi ya Urusi imesema chama kinachoiunga mkono Kremlin, cha United Russia kilishinda kwa urahisi uchaguzi wa serikali za mitaa.

tume hiyo imesema hali ilikuwa shwari katika maeneo yaliyonyakuliwa, kufuatia uchaguzi wa mwishoni mwa juma.

Hata hivyo,uchaguzi huo ulipuuzwa na Kiev na kukosolewa kwa udanganyifu mkubwa.