1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Annalena Baerbock aifuta ziara yake Djibouti

25 Januari 2024

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Annalena Baerbock ameshindwa kufika nchini Djibouti baada ya ndege ya serikali ya nchi yake aliyokuwa akisafiria kuknyimwa kibali cha kupaa kwenye anga ya Eritrea.

https://p.dw.com/p/4bej4
Saudi Arabia/ Baerbock
Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Annalena BaerbockPicha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Ndege ya Waziri Annalena Baerbock ililazimika kutua mjini Jeddah Saudi Arabia hapo jana ambako yeye pamoja na Ujumbe wake walikaa huko kwa siku moja na hii leo Alhamisi (25.01.2024), walitarajiwa kuendelea na safari yao kuelekea nchini Djibouti, lakini baadae wakaifutilia mbali safari hiyo.

Vyanzo katika ujumbe huo vimesema Baerbock ataendelea na ziara yake nchini Kenya kama sehemu ya ratiba ya ziara yake Afrika Mashariki. 

Baerbock ahimiza 'shinikizo' Sudan

Ndege ya Waziri huyo wa mambo ya nje wa Ujerumani ilitua mjini Jeddah saa nane na dakika kumi na tano mchana hapo jana (24.01.2024), baada ya kuzunguka katika anga ya Bahari ya shamu kwa zaidi ya saa moja.

Baada ya kutua Jeddah Baerbock alisema mambo yanapotokea ambayo hayakupangwa ni lazima uwe haraka wa kufanya maamuzi mengine na kwamba sio kila kitu kinaweza kwenda kama ilivyotarajiwa.

Ujerumani yashinikiza amani Sudan

Kufuatia pia mashambulizi yaliyoanzishwa na waasi wa Yemen wanaounga mkono na Iran wa Houthi dhidi ya meli katika bahari ya shamu, haikuwezekana kwa ndege ya mwanadiplomasia huyo kupaa katika anga ya Eritrea. 

Ziara yake ni ya kutafuta suluhu ya kisiasa katika mzozo wa Sudan

Sudan | Jenerali Fattah al-Burhan na Mohamed Dagalo
Kiongozi wa jeshi la Sudan Jenerali Abdel Fattah Abdelrahman al-Burhan na mwenzake kiongozi wa wanamgambo wa RSF Mohamed Hamdan Dagalo.Picha: Mahmoud Hjaj/AA/picture alliance

Kwa kawaida Baerbock alitarajiwa kuwa na mazungumzo nchini Djibouti, Kenya na Sudan Kusini ifikapo siku ya Ijumaa. Katika ziara hii alitaka kuwa wazi kabisa katika mataifa mengi jirani kwamba Ujerumani sio tu kwamba inawajali lakini pia haijawasahau watu wa eneo hilo hasa kwa kuzingatia vita nchini Sudan.

Alitarajiwa kukutana na Waziri wa mambo ya kigeni wa Djibouti Mahamoud Ali Youssouf hapo jana na alitaka pia kuwasilisha ujumbe kwamba Ujerumani  inachukua jukumu la kuwa na uhuru wa kuingia katika Bahari ya shamu na kusema kwamba hali katika eneo hilo inaleta ukosefu wa uthabiti kwa dunia na kanda nzima.

Sudan yamwondoa balozi wake Kenya baada ya ziara ya Dagalo

Alielezea pia mpango wa kijeshi uliopangwa na Umoja wa Ulaya wa kulinda meli za raia katika bahari hiyo, kama mchango muhimu wa udhabiti  wa kanda hiyo.

Baerbock aliondoka siku ya Jumatano na mipango ya kuitembelea Djibouti, Kenya na Sudan Kusini kwa mazungumzo ya kidiplomasia, yanayolenga kupata ufumbuzi wa mzozo kati ya pande mbili zinazohasiamiana Sudan, Kiongozi wa Kijeshi Abdul Fattah al Burhan na naibu wake ambaye pia ni kiongozi wa kundi la wanamgambo wa RSF Mohammed Hamdan Dagalo.

dpa/reuters/afp