1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaRwanda

Baerbock anasema kiwanda cha chanjo Rwanda ni hatua muhimu

18 Desemba 2023

Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock ameliahidi bara la Afrika msaada wa Ujerumani na Umoja wa Ulaya katika mapambano dhidi ya magonjwa ya miripuko na pia magonjwa mengine

https://p.dw.com/p/4aHpe
Waziri wa mambo ya nje wa Rwanda Vincent Biruta (Kushoto) na waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock (Kulia) wakiwa Kigali Desemba 18.12.2023
Waziri wa mambo ya nje wa Rwanda Vincent Biruta (Kushoto) na waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock (Kulia)Picha: Florian Gaertner/photothek/picture alliance

Wakati akianza safari kueleka Rwanda siku ya Jumapili, Waziri Baerbock alisema magonjwa hayatambui mipaka ya kitaifa au mabara na kwamba mshikamano wao pia unapaswa kuzingatia hayo. Baerbock ameongeza kuwa njia ya kufikia mfumo wa afya wa kimataifa wenye haki, sio mchakato wa muda mfupi, lakini wenye kuchukuwa hatua mbali mbali.

Waziri huyo wa kigeni wa Ujerumani amesema kuwa hii ndio sababu bara la Ulaya linaunga mkono lengo la utengenezaji chanjo barani Afrika kutoka mwanzo wake hadi mwisho.

Baerbock amesema utengezenezaji chanjo barani Afrika unapaswa kuongezeka

Baerbock amesema kuwa kwasasa, ni chanjo moja tu kati ya 100 zinazotolewa barani Afrika, iliyotengenezwa katika eneo hilo na kuongeza kuwa kufikia mwaka 2040, takwimu hii inapaswa kuwa mara 60 zaidi.

Mpango wa kimataifa wa Umoja wa Ulaya kuwekeza katika miradi ya miundombinu na kuanzisha ushirikiano wa kiuchumi, utawezesha hilo kwa msaada wa dola bilioni 1.3 kufikia mwaka 2027 kutoka Ujerumani.

Soma pia: Baerbock ziarani Rwanda kushuhudia uzinduzi wa kiwanda cha chanjo

Baerbock amesema kuwa kiwanda cha kwanza cha chanjo ya (mRNA) ya Uviko-19 nchini Rwanda, sio hatua ya mwisho lakini maendeleo makubwa na matumaini ya mamilioni ya watu.

Chanjo ya (mRAN) ya Uviko- 19
Chanjo ya (mRAN) ya Uviko- 19Picha: Steven Heap/Zoonar/picture alliance

Baerbock amesema wakati janga la Uviko-19 lilipoenea ulimwenguni, ulimwengu uligundua kuwa hakuna aliye salama hadi kila mtu atakjapokuwa salama. Ameongeza kuwa hali hiyo bado inaumiza hadi leo kwamba watu wengi sana, haswa barani Afrika, walishindwa kujikinga dhidi ya virusi hivyo hapo mwanzoni mwa janga hilo na kwamba wao kama jamii ya kimataifa, pia hawakuweza kusaidia.

Baerbock amesema ufikiaji chanjo haupaswi kufanywa kibaguzi

Baerbock amesisitiza kwamba, ufikiaji wa haki na wa haraka wa chanjo za kuokoa maisha haupaswi kutegemea kama mtoto amezaliwa Ujerumani au Rwanda. Chanjo kama hiyo dhidi ya ugonjwa wa malaria na kifua kikuu zina uwezekano pia wa kutengezwa barani Afrika katika siku zijazo ikiwa idhini itatolewa.

Soma pia:Rwanda yaanza ujenzi wa kiwanda cha chanjo ya Covid 19

Kulingana na Wizara ya Maendeleo ya Ujerumani, serikali mjini Berlin inaunga mkono kuanzishwa kwa utengezaji endelevu wa chanjo na dawa barani Afrika ili kusaidia kuliandaa bara hilo kwa majanga ya baadaye.

Historia ya Ujerumani Afrika Rwanda

Baerbock anatarajiwa kukutana na waziri wa mambo ya nje wa Rwanda Vincent Biruta

Baerbock anatarajiwa kuhudhuria ufunguzi wakiwanda cha kwanza cha chanjo ya (mRNA) ya Uviko-19 nchini Rwanda hii leo. Haya ni kulingana na afisi yake mjini Berlin.

Pia anatarajiwa kukutana na waziri wa mambo ya nje wa Rwanda Vincent Biruta mjini Kigali na kutembelea eneo la kumbukumbu ya wahanga wa mauaji ya kimbari dhidi ya  Watutsi.