1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Assange arejea nchini mwake baada ya kuachiliwa huru

26 Juni 2024

Ndege iliyombeba mwasisi wa mtandao wa WikiLeaks uliotumika kufichua siri za serikali za mataifa mbalimbali duniani Julian Assange imetua mji mkuu wa Australia wa shughuli za kiserikali, Canberra.

https://p.dw.com/p/4hX83
USA | Julian Assange
Assange arejea nchini mwake baada ya kuachiliwa huruPicha: YUICHI YAMAZAKI/AFP/Getty Images

Familia yake, akiwemo mkewe Stella Assange na babake John Shipton, wanaripotiwa kuwepo kwenye uwanja wa ndege kumpokea.
Assange ameachiwa huru baada ya kukiri shtaka la udukuzi na kujipatia taarifa kuhusu ulinzi wa taifa na kuzisambaza, chini ya mpango maalum aliofikia na Marekani. 

Assange aliachiwa kwa dhamana kutoka jela yenye ulinzi mkali ya  Kusini Mashariki mwa London siku ya Jumatatu. Mkewe Stella Assange alisema sasa mumewe ni mtu huru baada ya jaji wa Marekani kusaini kuridhia makubaliano ya kihistoria ya kisheria kati ya upande wa Mashtaka ambayo ni Marekani na mshtakiwa, ambapo alitarajiwa kukubali mashtaka hayo katika eneo la visiwa vya Northern Mariana ambalo liko chini ya himaya ya Marekani.

Baerbock akaribisha 'suluhisho' la kesi ya Assange

Stella Assange amesema hatimae huu ndio mwisho wa safari ndefu ya mapambano ya kisheria ya mumewe ambaye baada ya kuachiwa kwenye gereza la  Berlmash alifanikiwa kuchukuwa ndege kutoka London kuelekea Bangkok na hatiamae, Saipan, katika safari iliyojawa na hisia nyingi. 

Mwasisi huyo wa mtandao wa WikiLeaks Julian Assange,mwenye umri wa miaka 52 na raia wa Austarlia, amekaa  jela kwa miaka mitano akipambana kupinga kupelekwa Marekani,nchi ambayo ilitaka kumshtaki kwa kufichuwa nyaraka za siri za jeshi la taifa hilo.