1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Algeria yasubiri matokeo ya uchaguzi wa rais

7 Septemba 2024

Raia wa Algeria wanasubiri matokeo ya uchaguzi wa rais uliofanyika leo Jumamosi ambao utaamua mwanasiasa atakayeliongoza taifa hilo la kaskazini mwa Afrika kwa kipindi cha miaka mitano inayokuja.

https://p.dw.com/p/4kO3m
Rais Abdelmadjid Tebboune wa Algeria anawania muhula wa pili
Rais Abdelmadjid Tebboune wa Algeria anawania muhula wa pili.Picha: Photoshot/picture alliance

Zoezi la kupiga kura lilianza mapema saa mbili asubuhi saa za Algeria na lilihitimishwa saa kumi na moja jioni. Matokeo ya mwisho yanatarajiwa kutolewa kesho Jumapili.

Rais aliye madarakani Abdelmadjid Tebboune anatazamiwa kushinda muhula wa pili madarakani akiwashinda wapinzani wawe wawili. Wanaochuana naye ni Abdelaali Hassani anayegemea siasa za dini ya kiislamu na mgombea wa kambi ya wasoshalisti Youcef Aouchiche. 

Tebboune aliingia madarakani Disemba mwaka 2019 kiasi mwaka mmoja baada ya maandamano ya umma kumlazimisha aliyekuwa rais wa nchi hiyo Abdelaziz Bouteflika kujiuzulu. Anatumai safari hii raia wengi watajitokeza kupiga kura kufuatia idadi ndogo ya wapigakura katika uchaguzi uliopita.