1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika yabaki pake yake kupambana na majanga

12 Oktoba 2022

Kaimu mkuu wa vituo vya vya kudhibiti na kuzuia magonjwa barani Afrika Ahmed Ogwell amesema Afrika inatakiwa kushughulikia kikamilifu milipuko ya magonjwa bila ya kusubiri misaada ya kimataifa.

https://p.dw.com/p/4I5lT
Querschnitt I Ebola Virus
Picha: IMAGE POINT FR/NIH/NIAID/BSIP/picture alliance

Kaimu mkuu huyo aidha ameonya kwamba bara hilo lenye watu bilioni 1.3 linatakiwa kutambua huwa liko peke yake zinapofika nyakati za majanga. 

Ahmed Ogwell amesema kwa kuwa mara nyingi misaada haipatikani kwa wepesi, mataifa ya Afrika yanalazimika kuondoa pengo lililopo katika kukabiliana na milipuko ya magonjwa kama Ebola nchini Uganda.

Amesema, hapa namnukuu, "huu ni mlipuko wa kwanza hapa barani Afrika wa kirusi cha Ebola kilichoanzia Sudan na ni bahati mbaya kwamba kwa sasa bara hilo halijaweza kuvitambua virusi hivyo kwa haraka na wala hakuna chanjo yake.

Soma Zaidi:Kenya yajiweka sawa dhidi ya Ebola 

Uganda Ausbruch von Ebola
Waziri wa afya wa Uganda Diana Atwine akithibitisha kisa cha kwanza cha Ebola nchini humo mwishoni mwa mwezi Septemba.Picha: Hajarah Nalwadda/ASSOCIATED PRESS/picture alliance

Ogwell amesema hayo akiwa Kampala nchini Uganda ambako maafisa wa afya ya umma wa barani Afrika na wengineo wanakutana kupanga namna mataifa hayo yatakavyoshirikiana kukabiliana na Ebola.

litangaza mlipuko wa Ebola, Septemba 20.

Mataifa 54 ya Afrika bado hayajapata msaada wowote wa kuridhisha wa kimataifa kwa ajili ya kupambana na majanga ya karibuni ya kiafya, hii ikiwa ni kulingana na wataalamu na hata katika wakati wa janga la UVIKO-19 mataifa yalijikuta katika wakati mgumu.

Ogwell aidha aliilaumu jumuiya ya kimataifa kwa kushindwa kusaidia nchi za Afrika kuboresha uwezo wa kupima homa ya nyani pamoja na kudhibiti kuenea kwa homa hiyo iliyosababisha vifo vya watu wengi zaidi barani Afrika kwa mwaka huu kuliko kwingineko ulimwenguni.

DW Videostill | Uganda grapples with Ebola outbreak
Wakazi wa eneo la Madudu nchini Uganda wakiwa na simanzi baada ya kutangazwa mlipuko wa Ebola nchini humo.Picha: DW

Mlipuko wa Ebola ulianzia katika jamii inayoishi katikati mwa Uganda ambako watumishi wa afya hawakuweza kuutambua mapema. Mwanzoni maafisa waliuelezea kama "ugonjwa wa ajabu" unaowaua watu. Hadi sasa watu 54 wameambukizwa virusi vya Ebola na 19 wamekufa ikiwa ni pamoja na watumishi wa afya.

Soma Zaidi:Tanzania kuweka vituo vya udhibiti Ebola 

Si rahisi sana kuutambua ugonjwa huo kwa mara ya kwanza kwa sababu homa mara nyingine huwa ni dalili ya malaria. Majimaji ya mwilini huambukiza maradhi hayo inapotokea mwathirika anagusana na mtu mwingine. Dalili zake ni pamoja na homa, kutapika, kuharisha, maumivu ya misuli na wakati mwingine damu kuvuja ndani ama nje ya mwili.

Bado hakuna chanjo iliyothibitishwa ya kirusi hiki lakini mikakati inaendelea ya majaribio ya chanjo, inayofanywa na kikundi kidogo cha wataalamu wa Uganda waliokutana na wagonjwa.

Ogwell amesema kwa kuwa Ebola ndio ugonjwa wa kipaumbele cha sasa Afrika, kukosekana kwa utambuzi wa haraka na chanjo kunaamisha lipo ombwe katika kuweka vipaumbele kwenye magonjwa yanayolisumbua bara hilo pamoja na vifaa vinavyohitajika vya kupambana nao na kuongeza kuwa kama Afrika ni lazima sasa wafikirie tofauti hasa kwa kutambua kwamba mara nyingi wako peke yao.

Sikiliza zaidi: 

Mripuko wa Ebola nchini Kongo, tatizo liko wapi?

Mashirika:APE