1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ziara ya Scholz Afrika kuimarisha uhusiano wa kiuchumi

Iddi Ssessanga Isaac Kaledzi
1 Novemba 2023

Afrika imekuwa kivutio cha kimkakati na kiuchumi kwa Ujerumani. Chumi hiyo kubwa zaidi ya Ulaya inataka kuimarisha uhusiano, na ziara ya Olaf Scholz nchini Ghana na Nigeria ililenga kufanikisha hilo.

https://p.dw.com/p/4YIAi
Ghana| Kansea wa Ujerumani Scholz na Rais wa Gahan Nana Akufo-Addo
Kansea wa Ujerumani Scholz na Rais wa Gahan Nana Akufo-Addo.Picha: picture alliance/dpa

Ziara ya Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz nchini Nigeria na Ghana ambayo ilikuwa ya tatu Afrika katika kipindi cha miaka miwili ilikuwa na lengo la kuimarisha uhusiano wa kiuchumi kati ya Ujerumani na mataifa hayo mawili ya Afrika, huku bara hilo likizidi kuwa kivutio cha kimkakati na kiuchumi kwa Ujerumani.

Nigeria inakabiliwa na matatizo, huku thamani ya uchumi wake ikiripotiwa kushuka hadi dola bilioni 477 mwaka 2022 kutoka dola bilioni 546 bilioni mwaka 2015.

Soma pia: Ujerumani kufanya biashara ya nishati na Nigeria

Wakati wa mazungumzo ya pande mbili, rais wa Nigeria Bola Tinubu aliwavutia wawekezaji kwenye sekta ya madini ya nchi hiyo, ambayo imekuwa na maendeleo duni kwa miongo kadhaa. Pia alifichua majadiliano ambayo yalikuwa yamefanyika na kansela wa Ujerumani juu ya uwezekano wa kusafirisha gesi Ulaya.

Nigeria | Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz na Rais wa Nigeria Bola Ahmed Tinubu
Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz na Rais wa Nigeria Bola Ahmed Tinubu.Picha: Kola Sulaimon/AFP/Getty Images

"Uwezekano wa sekta ya nishati kuwezesha usafirishaji wa gesi ya kimiminika barani Ulaya umwejadiliwa vyema mapema. Tuna jicho letu kwenye hili," Tinubu alisema.

Makampuni ya Ujerumani yalilenga kukuza shughuli zao barani Afrika mwaka huu, hasa katika maeneo kama vile gesi ya hidrojeni ambayo ni rafiki kwa mazingira, na gesi asilia.

Wanachama wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Afrika na Ujerumani pia walionesha nia ya kustawisha viwango vyao vya matumizi barani Afrika.

Ongezeko la uwekezaji Afrika

Kansela Scholz pia aligusia suala hili. Eneo moja muhimu kwa uwekezaji unaotarajiwa alitaja: sekta ya nishati. Scholz alisema nchini Nigeria kwamba moja ya maeneo makuu ya ushirikiano kati ya Berlin na Abuja litakuwa "kutumia fursa za kiuchumi za taifa lako."

Alisema miongoni mwa fursa hizi zilikuwa "gesi na mafuta, ambazo kijadi zinahusishwa na nchi yako."

Soma pia: Ujerumani na Ulaya kusaidia kuimarisha usalama Afrika Magharibi

Kama taifa lenye uchumi mkubwa zaidi barani Ulaya, Ujerumani imekuwa ikitafuta kupunguza utegemezi wake kwa gesi ya Urusi tangu nchi hiyo ilipoivamia Ukraine, na inaitazama sekta ya nishati ya Afrika kama chaguo mbadala.

Nchini Ghana, ambayo ndiyo yenye uchumi wa pili kwa ukubwa Afrika Magharibi, mazungumzo ya Kansela Scholz na rais wa Ghana Nana Akufo Addo yalijikita pia kwenye kutanua uhusiano wa kiuchumi katika nyanja za nishati, kilimo na teknolojia ya kidigitali.

Mauzo ya Ujerumani kwenda Ghana katika mwaka wa 2022 yalikuwa dola milioni 314.77, lakini wataalamu wanaamini kuna uwezekano wa kuongeza biashara kati ya mataifa hayo mawili katika miaka ijayo.

Baadhi ya wachambuzi wanaizingatia Ujerumani kuwa mfadhili mkuu wa Umoja wa Afrika na shughuli zake. Sababu mojawapo ya hilo ni kazi ya shirika la ushirikiano wa kimataifa la Ujerumani, GIZ, ambalo lina programu kadhaa za kiuchumi kote barani Afrika.

Msaada wa kiuchumi wa Ujerumani Afrika

Mchambuzi wa masuala ya Afrika Emmanuel Bensen aliiambia DW kwamba ziara ya Scholz itaimarisha uwekezaji na kuiwezesha Ujerumani kuendelea kushikilia udhibiti kama huu barani Afrika.

"Nadhani sote tunafahamu ni kiasi gani GIZ katika miaka 10 iliyopita na zaidi, imesaidia katika masuala mengi ya Umoja wa Afrika, ECOWAS na taasisi nyingi za kanda hiyo," alisema.

Soma pia:Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz amalizia ziara yake katika nchi mbili za Afrika huko nchini Kenya. 

Aliongeza kuwa mkutano wa Scholz na viongozi wa Nigeria na Ghana, mataifa mawili yenye nguvu Afrika Magharibi, inapaswa kumuwezesha kutambua thamani athari ya programu za GIZ kwa watu halisi.

Paul Ejime, mchambuzi wa masuala ya kimataifa mwenye makao yake nchini Nigeria, alifafanua kwamba kuwa na bara tulivu inaendeleza ajenda ya Ujerumani na Magharibi.

Kansela wa Ujerumani afanya ziara ya kwanza barani Afrika

Soma pia: Kansela Scholz azungumza na Rais Ruto

"Hakuna nchi ya ulimwengu ya kwanza itakweda na kutupa pesa zao katika bara lisilo na utulivu kwa sababu uwekezaji huu unafuata utulivu na kisha unafuata maslahi. Unafuata faida kwa sababu ikiwa hauna faida yoyote kwenye uwekezaji, ikiwa hakuna faida kwenye uwekezaji, hupaswi kwenda huko," Ejime alisema.

Mradi wa Ujerumani wa "Compact with Africa" umekuwa kipengee muhimu cha uhusiano wake na bara hilo. Ndiyo kiini cha mifumo ya msaada wa uhamiaji na kusaidia kuwajumuisha tena Waafrika wanaotaka kurejea kutoka Ujerumani na Ulaya.

Ujerumani pia ilielezea uungwaji wake mkono wa demokrasia barani Afrika, na Scholz aliangazia hili wakati wa ziara yake katika sekriteriat ya jumuiya ya kiuchumi ya Afrika Magharibi, ECOWAS, ambako alizungumzia wasiwasi kuhusu idadi kubwa ya mapinduzi ya kijeshi katika bara la Afrika.