1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ziara ya Papa Francis ulimwengu wa Kiarabu

8 Februari 2019

Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Francis, alikuwa na ziara ya kihistoria ya siku tatu katika ulimwengu wa Kiarabu mapema Febuari. Aliwasili kwenye Umoja wa Falme za Kiarabu, ambako alilakiwa na mamia kwa maelfu ya waumini wa dini yake na wa Kiislamu. Je kwa kiasi gani safari ya Papa ilikuwa kiashirio cha uvumilivu wa kidini?

https://p.dw.com/p/3CzCX

Akizungumzia ziara yake hiyo, Papa Francis ameiita kama ukurasa mpya kwenye historia ya mdahalo baina ya Ukristo na Uislamu na katika kushajiisha amani duniani, iliyojikita kwenye misingi ya udugu. Mjini Abu Dhabi, Papa Francis alikutana pia na Imamu Mkuu wa Al-Azhar, Sheikh Ahmad el-Tayeb, -  Al Azhar iliyoko Misri ndiyo ichukuliwayo na waumini wa madhehebu ya Sunni kwenye Uislamu kama taasisi yenye nguvu kubwa kabisa upande wao.

Kipindi cha Maoni mbele ya Meza ya Duara kinaichambua ziara hiyo ya Papa Francis kwa muelekeo wa uvumilivu wa kidini. Kwa kiasi gani safari yenyewe ya Papa ilikuwa kiashirio cha uvumilivu huo? Kwa kiasi gani, dunia inaumizwa na ukosevu wa uvumilivu baina ya Ukristo na Uislamu? Na, juu ya yote, ziara kama hizi zinaweza kuashiria kipi huko twendako.

Washiriki ni wataalamu wa masuala ya mahusiano ya kijamii na kidini; bwana Mohammed Said kutoka Dar es Salaam, Tanzania, mwandishi wa masuala ya historia ya mahusiano baina ya jamii hizi mbili, Padri Maziku kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine, Mwanza, ambaye pia ni mhadhiri kwenye chuo hicho, Abdulfattah Mussa akiwa Tehran, mwandishi wa habari na mchambuzi wa masuala ya Ghuba na Mashariki ya Kati, na pia Padri Privatus Karugendo, kutoka Bukoba, Tanzania.