1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUkraine

Zelensky asema jeshi lake liko katika vita 'vikali' mpakani

13 Mei 2024

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema vikosi vyake vinapambana vikali katika maeneo mawili ya mipaka dhidi ya mashambulizi ya Urusi.

https://p.dw.com/p/4fmyt
Eneo la Volchansk, jimbo la Kharkiv | Juhudi za kuwaondoa watu baada ya shambulizi la Urusi
Jengo la makazi lililoharibiwa kwenye vita vya hivi karibuni katika viunga vya Volchansk jimbo la Kharkiv Ukraine mnamo Mei 11, 2024, kufuatia uvamizi wa Urusi.Picha: GEORGE IVANCHENKO/EPA

Vita hivyo vikali vinatokana na mashambulizi ya vikosi vya Urusi vinavyojaribu kusonga mbele katika vijiji vya mpaka wa jimbo la Kharkiv. 

Mashambulizi mapya ya Urusi Kaskazini mashariki mwa jimbo la Kharkiv, pamoja na msukumo wake unaoendelea katika mkoa wa mashariki Donetsk, vinajiri baada ya miezi kadhaa, kabla ya kutopiga hatua yoyote kwenye uwanja wa mapambano wa takriban kilomita 1,000.

Wakati huu, pande zote mbili zimefanya mashambulizi ya masafa marefu katika kile kimegeuka kuwa hatua za kuhujumu uwezo wa adui.

Uvamizi wa jimbo la Kharkiv unaweza kuwa jaribio la kuunda "eneo kinga" kulinda Belgorod, eneo la mpaka la Urusi linaloshambuliwa na Ukraine.

Soma pia: Vladmir Putin: Urusi haitaruhusu vitisho

Kauli ya rais Zelensky imejiri wakati idadi ya vifo kwenye jengo lililoporomoka nchini Urusi, shambulizi lililodaiwa kufanywa na Ukraine, ikiongezeka na kufikia watu 15.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky
Rais wa Ukraine Volodymyr ZelenskyPicha: Gints Ivuskans/AFP

Wachambuzi Urusi yaidhoofisha Ukraine kabla ipate msaada wa kijeshi

"Vita vya ulinzi na mapigano makali yanaendelea katika sehemu kubwa ya mpaka wetu. Kuna vijiji ambavyo vimegeuzwa maeneo ya mapigano na mvamizi anajaribu kuchukua udhibiti wa baadhi yao ili kuvitumia katika juhudi zake kusonga mbele zaidi,” amesema Zelensky.

Soma pia: Putin aamuru mazoezi ya silaha za nyuklia karibu na Ukraine

Wachambuzi wanasema vikosi vya Urusi vinalenga kutumia udhaifu wa Ukraine kabla msaada mkubwa mpya wa kijeshi kutoka Marekani na washirika wake wa Ulaya uwafikie katika uwanja wa mapambano.

Kulingana na wachambuzi hali hiyo inakifanya kipindi hiki cha vita kuwa fursa muhimu kwa Urusi, lakini hatari zaidi kwa Ukraine, kwenye vita hivyo ambavyo vimedumu kwa miaka miwili sasa.

Putin amuondoa Sergei Shoigu kuwa waziri wa Ulinzi

Katika tukio jingine, rais wa Urusi Vladimir Putin amefanya mabadiliko kwenye baraza lake la mawaziri na kumbadilisha waziri wake wa Ulinzi Sergei Shoigu.

Urusi | Vladimir Putin na Sergei Shoigu kwenye gwaride la kijeshi la Siku ya Ushindi huko Moscow Mei 09, 2024
Rais wa Urusi Vladimir Putin amuondoa Sergei Shoigu kama waziri wa UlinziPicha: Alexander Zemlianichenko/AP Photo/picture alliance

Ikulu ya Kremlin imeeleza kuwa Shoigu badala yake ameteuliwa kuwa katibu wa Baraza la Usalama la Urusi.

Putin amemteua Andrei Belousov, naibu waziri mkuu wa zamani ambaye amebobea katika masuala ya uchumi, kuwa waziri mpya wa ulinzi.

Belousov hata hivyo atahitaji kuidhinishwa na bunge.

Soma pia: Urusi yaionya Ufaransa fikra ya kupeleka wanajeshi Ukraine

Kwa mujibu wa sheria ya Urusi, Baraza lote la Mawaziri lilijiuzulu siku ya Jumanne baada ya kuapishwa kwa Putin japo mawaziri wengi walitarajiwa kuhifadhi nafasi zao.

Shoigu aliteuliwa kuhudumu kama waziri wa ulinzi mwaka 2012, miaka miwili kabla ya Urusi kulinyakua jimbo la Ukraine la Crimea.

Alitizamwa kuwa na ushawishi mkubwa katika uamuzi wa Putin kuivamia Ukraine mnamo Februari 2022.

Kutibu majeraha yaliosababishwa na vita Ukraine

Vyanzo: APE, AFPTV