1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiIndia

Karibu watu 105 wafa kwenye mkanyagano nchini India

2 Julai 2024

Karibu watu 100 wamekufa katika mkanyagano kwenye kusanyiko la kidini katika jimbo la kaskazini mwa India la Uttar Pradesh, katika moja ya tukio baya kabisa kuwahi kutokea katika miaka ya karibuni.

https://p.dw.com/p/4hmw7
India I Waumini wafa kwa mkanyagano
Baadhi ya watu wakiomboleza karibu na mwili wa jamaa yao nje ya hospitali ya Sikandrarao katika wilaya ya Hithras kusinimagharibi mwa India, Julai 2, 2024Picha: Manoj Aligadi/AP/picture alliance

Tukio hili la mkanyagano limetokea kwenye kijiji kilichopo wilaya ya Hathras karibu kilomita 200 kusinimashariki mwa mji mkuu wa India, New Delhi ambako mamlaka zimesema kulikuwa na kusanyiko kubwa kwenye eneo la wazi lililoitishwa na kiongozi wa kidini kwa ajili ya tamasha la waumini wa Hindu wakimkumbuka mungu wao wa Shiva, katika jiji la Hathras.

Hili si tukio pekee la mkanyagano lililowahi kutokea nchini humo, bali taifa hilo limeshuhudia matukio mengine kama haya kwenye mikusanyiko ya kidini:

JANUARI 2005: Zaidi ya waumini 265 wa madhehebu ya Hindu walikufa na wengine mamia walijeruhiwa katika mkanyagano kwenye hekalu ya Mandhardevi katika mji wa Wai magharibi mwa jimbo la Maharashtra. Mkanyagano huo ulisababishwa na mterezo kwenye ujia wa kuingilia hekaluni, hii ikiwa ni kulingana na vyombo vya habari kwa wakati huo.

AGOSTI 2008: Kulitokea mkanyagano kwenye hekalu ya Naina Devi lililopo kilimani kwenye jimbo la kaskazini mwa India la Himachal Pradesh. Mahujaji 145 wa Hindu walikufa na kulikuwa na minong'ono kwamba mkanyagano huo ulisababishwa na maporomoko ya ardhi.

Majanga nchini India
Jeshi la polisi na wapita njia wakiwa wamekusanyika kwenye daraja ambako waumini wa Hindu walikanyagana nje ya hekalu ya Ratangarh kwenye wilaya ya Datia, jimbo la Madhya Pradesh, Oktoba 13, 2013 ambako watu waliokufa walifikia 109.Picha: STR/AFP/Getty Images

SEPTEMBA 2008: Jumla ya watu 250 walinusurika kufa kwenye hekalu ya Chamundagar iliyoko jimbo lenye ukame mkubwa la kaskazini mwa India la Rajastahn. Mahujaji hao walikusanyika kusherehekea tamasha la kila mwaka la madhehebu ya Hindu la Navratri kwa heshima ya mungu, Durga. Tamasha hilo huadhimishwa kwa siku tisa.

Soma pia: Watu 50 wauawa, zaidi ya 200 wajeruhiwa kwenye mkanyagano

MACHI 2010: Karibu watu 63, nusu yao wakiwa ni watoto walikufa katika mkanyagano uliochochewa na kugombania mgao wa chakula na mavazi ya bure katika hekalu ya Hindu katika jimbo la Uttar Pradesh kaskazini mwa India. Watu hao walikusanyika ili kujipatia chakula na nguo kwenye eneo hilo, viliripoti vyombo vya habari.

FEBRUARI 2013: Karibu mahujaji 36 wa madhehebu ya Hindu walikufa kwenye mkanyagano katika siku yenye shughuli nyingi zaidi ya Kumbh Mela, mkusanyiko ambao huwakutanisha mahujaji milioni 100 katika kipindi cha miezi miwili kwenye jimbo hilohilo la Uttar Pradesh mnamo mwaka 2013. Miongoni mwa waliokufa ni wanawake 27 na msichana wa miaka 8.

NOVEMBA 2013: Karibu watu 115 walikufa na zaidi ya na zaidi ya 100 walijeruhiwa kwenye mkanyagano katika hekalu la Ratangarh iliyoko katika jimbo la Madhya Pradesh, katikati mwa India, ambako zaidi ya watu 150,000 walikusanyika kuadhimisha sikukuu ya Navratri 

JANUARI 2022: Karibu watu 12 walikufa na wengine walijeruhiwa katika mkanyagano kwenye eneo takatifu la Vaishno Devi huko Jammu na Kashmir, baada ya kusanyiko kubwa la waumini kujaribu kuingia kwenye eneo hilo kupitia ujia mwembamba.

Soma pia: Netanyahu abebeshwa lawama juu ya tukio baya la mkanyagano la mwaka 2021