1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaGambia

Waziri wa zamani wa Gambia kupandishwa kizimbani Uswisi

8 Januari 2024

Kesi inayomkabili waziri wa zamani wa mambo ya ndani wa Gambia aliyehudumu enzi ya utawala wa dikteta Yahya Jammeh inafunguliwa leo Jumatatu kwenye mahakama moja nchini Uswisi.

https://p.dw.com/p/4ayGa
Jengo la mahakama kwenye mji wa kusini mwa Uswisi wa Bellinzona
Baba Hydara, (wa pili kushoto) mtoto wa mwandishi wa habari wa Gambia aliyeuawa Deyda Hydara, akisimama mbele ya mahakama ya juu akiwa pamoja na wanaharakati wa kutetea haki za binadamu Picha: Julian Stratenschulte/dpa/picture-alliance

Kesi hiyo yenye mashtaka ya uhalifu dhidi ya ubinadamu inamkabili Ousman Sonko ambaye alikuwa waziri tangu mwaka 2006 hadi 2016.

Anatuhumiwa kusimamia mashambulizi ya kupangwa yaliyotekelezwa na vyombo vya usalama vya Gambia kwa lengo la kuwanyamazisha wapinzani wa utawala wa Jammeh.

Soma pia: Adama Barrow aahidi kuweka ukomo wa muhula wa urais Gambia 

Anahusishwa pia kufanya mauaji ya kukusudia, kuwatesa watu, kufanya ubakaji na kwa makusudi kuwanyima watu haki zao za msingi.

Iwapo atatiwa hatiani anaweza kuhukumiwa kifungo cha maisha gerezani.

Kesi yake inayosikilizwa kwenye mahakama ya makosa ya jinai kwenye mji wa kusini mwa Uswisi wa Bellinzona ilifunguliwa chini ya misingi ya kimataifa ya utoaji haki ambayo inaruhusu taifa la kigeni kuwashtaki na kuwahukumu watu wanaohusishwa na makosa ya kivitia, mauaji ya kimbari na uhalifu dhidi ya ubinadamu.