1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Janga

Watu wasiopungua 10 wafa katika moto wa nyika Chile

3 Februari 2024

Chile imetangaza hali ya hatari Ijumaa huku maafisa wakisema watu 10 wanahofiwa kufariki kutokana na moto wa msitu katika eneo la kati la Valparaiso, ambapo moto huo unatishia mamia ya nyumba.

https://p.dw.com/p/4bzoa
Moto Chile | Majirani wakitazama moto wa msituni ukiteketeza majengo huko Vina del Mar, Chile.
Majirani wakitazama moto wa msituni ukiteketeza majengo huko Vina del Mar, Chile, Ijumaa, Februari 2, 2024.Picha: Cristobal Basaur/AP/picture alliance

Maafisa wa eneo hilo walitoa idadi hiyo "ya awali" huku Rais wa Chile Gabriel Boric akitangaza "hali ya hatari kutokana na maafa, ili kuwa na rasilimali zote muhimu" za kukabiliana na moto huo.

Moto huo umejikita katika maeneo ya watalii ya Vina del Mar na Valparaiso, ambapo umeharibu mamia ya hekta za misitu na kuwalazimisha watu kuhama. Takriban hekta 480 tayari zimeteketezwa huko Valparaiso pekee, kulingana na CONAF, mamlaka ya kitaifa ya misitu ya Chile.

Soma pia: Ugiriki yapambana na mioto mikubwa ya msituni

Moto huo unasababishwa na joto kali la kiangazi na ukame unaoathiri eneo la kusini mwa Amerika Kusini unaosababishwa na hali ya hewa ya El Nino, huku wanasayansi wakionya kuwa sayari inayoongezeka joto imeongeza hatari ya majanga ya asili kama vile joto kali na mioto.

Huku Chile na Colombia zikipambana na ongezeko la joto, wimbi la joto linatishia kuzikumba Argentina, Paraguay na Brazil katika siku zijazo.