1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watu saba wameuawa katika eneo la machafuko Nigeria

4 Aprili 2022

Takribani watu saba wameuwa katika jimbo la Plateau nchini Nigeria ambako ghasia kati ya wafugaji wa Kiislamu na wakulima wa Kikristo zimekuwa zikitokea mara nyingi.

https://p.dw.com/p/49QDo
Nigeria Angriff von Nomaden im Bundesstaat Plateau | Sicherheitskräfte
Picha: Reuters/Reuters TV

Kiongozi wa wazee na duru za kiusalama zimeeleza kuwa wakaazi wa kijiji cha Chando Zerreci kwenye mji wa Bassa walikuwa wakiadhimisha tamasha la kila mwaka Jumamosi usiku wakati waliposhambuliwa na watu wenye silaha.

Msemaji wa jumuia ya wakulima ya Kikristo, Davidson Malison amesema kijiji hicho kilishambuliwa na wanamgambo wa Fulani ambako watu 10 wamethibitishwa kuuawa.

Afisa usalama amethibitisha shambulizi hilo, lakini amesema watu saba ndiyo wameuawa. Malison anayewakilisha watu wa kabila la Irigwe amesema watu wengine wawili waliuawa jana asubuhi.

Kiongozi wa kabila la Fulani ambao ni wafugaji, Malam Nuru Abdullahi amekanusha kuwashambuliwa watu wa Irigwe, akisema badala yake watu wawili wa Fulani wameuawa pamoja na ng'ombe 90.