1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Washukiwa 4 wa mauji ya rais wauwawa Haiti.

8 Julai 2021

Kufuatia mauwaji ya Rais wa Haiti Jovenel Moise, polisi nchini humo imesema washukiwa wanne wameuwawa na wengine wawili kutiwa mbaroni. Umoja wa Mataifa umeonya dhidi ya uchochezi wowote zaidi wa vurugu nchini humo.

https://p.dw.com/p/3wCqP
Weltspiegel 8.7.2021 | Haiti
Picha: Joseph Odelyn/dpa/picture alliance

Katika hatua nyingine Umoja wa Mataifa umelaani mauwaji hayo katika kipindi hiki ambacho waziri mkuu wa taifa hilo na baraza lake la mawaziri wanashika hatamu ya uongozi hadi pale utakapoitishwa uchaguzi mpya.

Vikosi vya usalama vya Haiti Jana Jumatano vimekabiliana vikali kwa silaha za moto na washambuliaji ambao watajwa kuhusika na mauwaji ya Rais Jovenel Moise, katika tukio lilitokea usiku wa kuamkia jana hiyo, mkasa ambao umelitumbukiza taifa hilo masikini katika mgogoro mkubwa zaidi.

Haiti | Ermordung Präsident Jovenel Moise
Polisi ya Haiti ikiwa katika operesheniPicha: Valerie AFP/Getty Images

Akizungumza kupitia televisheni, Mkuu wa Jeshi la Polisi Leon Charles amesema watu wanne wameuawa na wengine wawili kukamatwa baada ya mauaji hayo na kuongeza kuwa  polisi watatu walikamatwa kwa muda lakini wameachiliwa huru. Amesema polisi haitapumzika mpaka ihakikishe kwamba imewashughulikia wale wate waliohuisika na uovu huo. Leon amesema "Kwa wakati huu inavyozungumza nanyi polisi ipo katika makabiliano. Tumewazua njiani wakati wakitoroka katika eneo la tukio. Tangu wakati huo tunakabiliana nao. Watauwawa au kutiwa mbaroni."

Serikali yatangaza wiki mbili za dharura nchini Haiti.

Serikali ya Haiti imetangaza wiki mbili za dharura kwa shabaha ya kufanikisha zoezi la kuwatia mbaroni washukiwa wa mkasa huo, lakini pia Waziri Mkuu wa muda Claude Joseph akiwa kandoni mwa mkuu huyo wa polisi alisema "Tunasonga mbele pamoja, tunataka kujikomboa kutoka katika mgogoro huu ambao umekuwepo kwa muda mrefu. Umma unataabika kwa hali hii. Kwa mamluki, watambue kwamba polisi ya Haiti imewazingira. Hii ni habari nzuri kwa Asubuhi ya Alhamis hii, kitendo hiki cha kinyama hakiwezi kuachwa bila ya kuadhibiwa"

Viongozi mbalimbali duniani wameshutumu mauaji hayo, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kadhalika limeyalaani mauwaji hayo na kutoa wito kwa vyama vyote vya siasa nchini humo kuwa vistahamilivu ili kuepusha kulitumbukiza taifa hilo katika machafuko zaidi.

Moise alyekuwa na umri wa miaka 53 na kuingia madarakani 2017 aliuawa usiku wa Jumatano kwenye makazi yake karibu na mji mkuu Port-au-Prince. Kikundi cha watu wasiojulikana, walivamia nyumbani kwake na kumuuwa kwa kumpiga risasi Moise. Mkewe Martine kujeruhiwa vibaya..

Vyanzo: RTR