1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanasayansi: kirusi kipya cha Mpox kinabadilika kwa haraka

27 Agosti 2024

Wanasayansi wanaochunguza aina mpya ya kirusi cha Mpox ambacho kimesambaa nje ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, wanasema kirusi hicho kinabadilika haraka kuliko ilivyodhaniwa.

https://p.dw.com/p/4jyT5
Vipimo vya Mpox
Vipimo vya MpoxPicha: Dado Ruvic/Illustration/REUTERS

Wanasayansi kadhaa kutoka Afrika, Ulaya na Marekani wameliambia shirika la habari la Reuters kwamba kuna mambo mengi yasiyojulikana kuhusu kirusi chenyewe, ukali wake, na jinsi kinavyoambukiza kinazidi kufanya ufuatiliaji wake kuwa mgumu.

Mpox, ambao zamani ulijulikana kama homa ya nyani, umekuwa tatizo la afya ya umma kwenye baadhi ya maeneo ya Afrika tangu mwaka 1970, lakini haukuangaziwa kimataifa, hadi ulipoenea ulimwenguni mwaka 2022, hatua iliyosabbabisha Shirika la Afya Duniani, WHO kutangaza dharura ya afya ya umma kimataifa. Dharura hiyo iliondolewa miezi 10 baadae.

Soma: Ulaya kuzalisha chanjo zaidi za ugonjwa wa homa ya nyani

Aina mpya ya kirusi cha Mpox kinachojulikana kama Clade 1b, kimepewa umakini mkubwa tena kimataifa baada ya WHO kutangaza dharura mpya ya kiafya. Kirusi cha sasa kinaambukiza kwa kugusana na wanyama waliombukizwa, ambacho kimekuwa kikiienea Kongo kwa miongo kadhaa. Mpox kwa kawaida inasababisha dalili kama vile mafua na vidonda vyenye usaha na inaweza kuuwa.

Pakistan | Mpox
Abiria wakikaguliwa kubaini Mpox huko PakistanPicha: PPI/ZUMAPRESS/picture alliance

Kulingana na WHO, Kongo imerekodi zaidi ya visa 18,000 vya Mpox vinavyodhaniwa kuwa kirusi cha clade 1 na clade 1b na vifo 615 mwaka huu. Pia pamekuwepo na visa 222 vilivyothibitishwa vya kirusi cha clade 1b kwenye nchi nne za Afrika mwezi uliopita, pamoja na kisa kimoja nchini Sweden na Thailand, kwa watu waliosafiri kutokea Afrika.

Dokta Dimie Ogoina, mtaalam wa magonjwa ya kuambukiza katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Niger Delta nchini Nigeria, anasema ana wasiwasi Afrika inafanya kazi bila kufikiri. Dokta Ogoina ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya dharura ya WHO kuhusu homa ya Mpox, anasema alitoa tahadhari kwa mara ya kwanza mwaka 2017 kuhusu uwezekano wa maambukizi ya Mpox kwa njia ya ngono, ambayo sasa ni moja ya njia inayokubalika ya kuenea kwa virusi hivyo.Chanjo elfu kumi za Mpox zinatarajiwa kuwasili Afrika juma lijalo

Dokta Miguel Paredes, ambaye anachunguza mabadiliko ya Mpox na virusi vingine katika Kituo cha Saratani cha Fred Hutchinson huko Seattle, Marekani, anabainisha kuwa virusi vinavyosababisha Mpox kwa kawaida vimekuwa thabiti na vinabadilika polepole, lakini mabadiliko yanayoendeshwa na APOBEC yanaweza kuharakisha mabadiliko ya virusi.

Dokta Salim Abdool Karim, mtaalamu wa magonjwa wa Afrika Kusini, na mwenyekiti wa kamati ya ushauri ya Kituo cha Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa barani Afrika, CDC anasema kubadilika kwa virusi vya clade 1b na 11b, kunaweza kuchukuliwa kama ugonjwa wa zinaa.

Mgonjwa wa Mpox nchini Kongo
Mgonjwa wa Mpox nchini KongoPicha: Ruth Alonga/DW

WHOinasema kuwa watoto, wajawazito na watu wenye kinga dhaifu wanaweza kuwa katika hatari kubwa zaidi kuambukizwa Mpox na hata kufariki.

Utafiti zaidi unahitajika haraka, lakini timu tatu zinazofuatilia mripuko wa Mpox barani Afrika, zinasema haziwezi kupata kemikali zinazohitajika kwa ajili ya vipimo vya uchunguzi. Wanasayansi wanasema mipango inayotakiwa katika kukabiliana na homa hiyo ni pamoja na mikakati ya chanjo, bila hilo hali itakuwa ngumu zaidi.

Dokta Karim anasema takribani nusu ya visa vya mashariki ya Kongo, ambako kirusi cha clade 1b kimeenea sana, vinatambuliwa tu na madaktari, bila uthibitisho wa maabara. Anasema kupeleka vipimo maabara ni vigumu kwa sababu ya mfumo wa huduma ya afya ambao tayari ni dhaifu. Na kiasi cha watu 750,000 wameyakimbia makaazi yao kutokana na mapigano kati ya waasi wa M23 na vikosi vya serikali.Kampuni ya Bavarian Nordic kutengeneza dozi 440,000 ya mpox

Dokta Emmanuel Nakuone, mtaalamu wa Mpox katika Taasisi ya Pasteur mjini Bangui, Katika Jamhuri ya Afrika ya Kati, anasema maabara nyingi za Kiafrika haziwezi kupata vifaa vinavyohitajika. Kwa mujibu wa Dokta Nakuone, maabara bora ni muhimu kwa sababu ya kufuatilia miripuko ya magonjwa yanayosababisha vifo.