1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanamgambo wa kikurd walihama eneo linalopakana na Uturuki

Oumilkheir Hamidou
23 Oktoba 2019

Waziri wa ulinzi wa Marekani Mark Esper amewasili Baghdad ambako atatakiwa ajibu kwa muda gani wanajeshi wa Marekani waliolihama eneo la kaskazini mashariki mwa Syria wanapaga kusalia nchini Iraq.

https://p.dw.com/p/3RlVo
Irak | US Truppen auf Rückzug aus Syrien
Picha: Getty Images/B. Smith

Waziri wa ulinzi wa Marekani amepangiwa kukutana na waziri mwenzake sawa na waziri mkuu Adel Abdul Mahdi kuzungumzia mpango wa kuwaondowa wanajeshi wa Marekani nchini Syria na nafasi inayoweza kushikiliwa na Iraq katika mpango huo.

Viongozi wa kijeshi wa Iraq walisema hapo awali wanajeshi wa Marekani wanaovuka mpaka na kuingia Iraq kama sehemu ya hatua za kuihama Syria hawana ruhusa ya kubakia na kwamba wataweza kusalia huko kwa muda tu.

Ziara ya waziri wa ulinzi wa Marekani inafuatia pia makubaliano yaliyofikiwa Sochi kati ya rais Recep Tayyip Erdogan wa Uturuki na rais Vladimir Putin wa Urusi yanayozungumzia juu ya kuwekwa wanajeshi wa nchi hizo mbili kaskazini mashariki mwa Syria ili kuwaondowa wapiganaji wa kikurd na silaha zao kutoka mpaka wa Uturuki.

Wakimbizi wa  kikurd wa Syria wakipiga kambi karibu na mji wa Semalka
Wakimbizi wa kikurd wa Syria wakipiga kambi karibu na mji wa SemalkaPicha: Reuters/M. Hamed

Wakaimbizi wa Syria kurejeshwa katika eneo salama kaskazini mashariki mwa Syria

Masaa machache baada ya makubaliano hayo kutangazwa, wizara ya ulinzi ya Uturuki ilisema Marekani imeiarifu Uturuki kuhusu kukamilika zoezi la kuhama wanamgambo wa kikurd katika lile eneo la Usalama Uturuki inalodai litengwe kaskazini mwa Syria.

Kukamilika zoezi la kuhama wanamgambo wa kikurd YPG, kama kutathibitishwa, itamaanisha ushindi kwa rais Erdogan aliyeanzisha  Oktoba tisa iliyopita hujuma za kijeshi  ili kuwatimua wanamgambo hao kutoka eneo la karibu na mpaka wake na kufungua eneo salama kwaajili ya wasyria watakaorejeshwa nyumbani."

Makubaliano kati ya Uturuki na Urusi yaliyofikiwa katika mji wa mwambao wa bahari nyeusi-Sochi yanaidhinisha pia mpango wa kurejea wanajeshi wa rais Bashar al Assad katika eneo la mpakani kwa ushirikiano pamoja na vikosi vya Urusi, wakikamata nafasi ya vile vikosi vya Marekani vilivyokuwa vikipiga doria kwa miaka kadhaa katika eneo hilo pamoja na washirika wao wa kikurd.

Urusi imeonya wanamgambo wa kikurd watakaosalia katika eneo hilo la kaskazini mashariki mwa Syria ambalo litakuwa likisimamiwa na wanajeshi wa Urusi na Uturuki "watavunjwa nguvu".

Makubaliano kati ya Uturuki na Urusi yanatarajiwa kuanza kuifanya kazi jumatano mchana.

 

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AP/Reuters/dpa

Mhariri: Iddi Ssessanga