1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Walibya wataka mipasuko ikome na uchaguzi ufanyike

Josephat Charo
20 Juni 2024

Koury amesema Walibya wengi aliozungumza nao waliashiria umuhimu wa mkataba au makubaliano yatakayohakikisha pande zinazohasimiana zinaheshimu matokeo ya uchaguzi huo.

https://p.dw.com/p/4hHMR
Walibya wanataka uchaguzi ufanyike nchini mwao
Walibya wanataka uchaguzi ufanyike nchini mwaoPicha: Hazem Turkia/AA/picture alliance

Umoja wa Mataifa unasema raia wa Libya wanataka mipasuko nchini mwao ikome na wanasiasa wanaohasimiana waandae uchaguzi.

Naibu mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa kwa ajili ya Libya Stephanie Koury ameliambia baraza la usalama la Umoja wa Mataifa kwamba Walibya kutoka matabaka mbalimbali na maeneo yanayohasimiana wamechoshwa na migawanyiko inayoshuhudiwa nchini mwao na wanataka wadau wa siasa wautafutie ufumbuzi mkwamo wa muda mrefu na wakubaliane kuandaa uchaguzi wa kitaifa.

Soma pia: Mjumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Libya ajiuzulu

Koury ameliambia baraza la usalama amekuwa akikutana na viongozi wa siasa, wawakilishi wa mashirika ya kijamii, wasomi, makundi ya wanawake, viongozi wa kijeshi na wengine katika maeneo yanayohasimiana ya mashariki na magharibi kuwasikiliza maoni yao.

Amesema kuna makubaliano kwamba hali ya sasa haikubaliki na lazima ibadilike kuelekea uchaguzi na pande zote zitakuwa na wajibu wa kuyaheshimu matokeo.