1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wajerumani wagawanyika kuhusu wahamiaji

Isaac Gamba
7 Septemba 2018

Utafiti  uliochapishwa nchini Ujerumani unaonesha  mgawanyiko kati ya wakazi wa miji ya mashariki na miji ya magharibi nchini humo kuhusiana  na jinsi serikali inavyoshughulikia suala la wahamiaji.

https://p.dw.com/p/34TBw
Chemnitz
Picha: picture-alliance/dpa/R. Hirschberger

 Mjadala huo unaohusiana na hatua ya Kansela wa Ujerumani Angela Merkel kufungua milango kwa ajili ya wahamiaji  umeibuliwa tena wiki iliyopita baada ya  wafuasi wa siasa za mrengo wa kulia kuandamana kufuatia kuchomwa kisu mwanaume mjerumani mwenye umri wa miaka 35 August 26 katika mji wa mashariki wa Chemnitz . Wanaume  wawili mmoja raia wa Iraq na mwingine wa Syria wametiwa mbaroni wakihusishwa na shambulizi hilo.

Hata hivyo   maandamano hayo  yalijibiwa haraka na kundi lingine la waandamanaji waliokuwa wakiyapinga.

Hayo yanajiri mnamo wakati mkuu wa shirika la ujasusi wa ndani nchini Ujerumani Hans Georg Maassen   akionesha mashaka kuhusiana na taarifa zinazodai kwamba  wafuasi wa siasa za mrengo wa kulia walikuwa  wakiwakimbiza wageni  wakati wa maandamano yaliyofanyika katika mji huo wa Chemnitz, hiyo ikiwa ni kwa mujibu wa gazeti la Bild katika taarifa yake leo Ijumaa.

Akitolea mfano wa vidio inayosambaa mtandaoni inayoonesha  wafuasi wa mrengo wa kulia  wakiwafukuza watu walioonekana kuwa sio wajerumani, Maassen alisema hakuna ushahidi unaodhihirisha kuwa  vidio hiyo ni ya kweli.

Ameongeza kuwa idara yake inayohusika na kulinda katiba haina taarifa kuwa kitendo kama hicho kilifanyika  na kusisitiza kuwa kuna sababu za msingi za kuamini kuwa habari hizo zilikuwa za upotoshaji wa makusudi za kuufanya umma uache kufuatilia kisa cha mauaji ya mjini mjini Chemnitz.

Hans-Georg Maaßen
Hans - Georg Maassen mkuu wa shirika la ujasusi wa ndani UjerumaniPicha: picture-alliance/dpa/S. Stache

 

Raia kadhaa wa mataifa yakigeni wadai kuandamwa

Wakati wa maandamano ya awali August 26 mwandishi mmoja  wa habari wa kujitegemea wa gazeti la Die Zeit alichapisha vidio mbili mtandaoni  zikionesha waandamanaji wakiwafukuza  watu wanaonekana kuwa na asili ya kigeni. Polisi wanasema watu kadhaa wakiwemo wabulgaria,wasyria na waafghanistan walidai walivamiwa na waandamanaji.

Hivi karibuni Maassen alibanwa kufuatia mkutano wake na wafuasi wa chama kinachopinga wahamiaji nchini Ujerumani chama mbadala kwa ujerumani  (AfD).

Kitabu kilichoandikwa  na mmoja wa wanachama wa zamani wa chama cha AfD kinadai kuwa katika moja ya mikutano hiyo  iliyomshirikisha  mwenyekiti wa zamani wa chama cha AfD Frauke Petry, Maassen aligusia  jinsi ya kukwepa kufuatiliwa na shirika la ujasusi wa ndani nchini Ujerumani.

Aidha waziri mkuu wa serikali ya jimbo la Saxony, Michael Kretschmer amesema pia kuwa maandamano hayo ya wafuasi wa mrengo wa kulia   hayakuwa dhidi ya wahamiaji.

Hata hivyo kauli hiyo inakinzana na matamshi yaliyotolewa na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel anayesema kuwa vidio inayosambaa mtandaoni inaonesha jinsi maandamano hayo yalivyolenga kuonesha chuki dhidi ya wageni na kusisitiza kuwa vitendo hivyo havina nafasi chini ya utawala wa sheria.

Mshukiwa wa tatu katika mauaji hayo dhidi ya mwanaume wa Kijerumani mjini Chemnitz bado anatafutwa.

Mwandishi: Isaac Gamba /Dw

Mhariri      : Gakuba, Daniel