1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wadau wahimizwa kukitumia Kiswahili katika tafiti

Salma Said5 Julai 2023

Wataalamu wa lugha ya Kiswahili wametakiwa kuhakikisha wanatumia taaluma yao katika tafiti zao badala ya kutumia lugha za kigeni ambazo mara nyingi ndio hutumika katika utafiti.

https://p.dw.com/p/4TSd4
Zanzibarl Siku ya Kiswahili 2023
Wadau wakishiriki mjadala wa wazi kuhusu matumizi ya Lugha ya Kiswahili uliofanyika ZanzibarPicha: Salma Said/DW

Mbali na kutakiwa kuitumia katika tafiti lugha ya Kiswahili wito pia umetolewa wa kukipenda Kiswahili na kukithamini sio tu kwenye mikutano ya kisiasa bali katika mazingira yote ya maisha ambayo wataalamu na watumiaji wa Kiswahili wanakutana nayo.

Kongamano la Kiswahili Zanzibar

Wito huo umetolewa katika mjadala wa wazi ambao umewashirikisha watumiaji wa misamiati ya Kiswahili na watafiti kutoka vyuo vikuu vya ndani na nje ya nchi wakati wa kujadili mada isemayo Kiswahili nyenzo ya ukombizi wa fikra kwa maendeleo ya kiuchumi Barani Afrika.

Professa Amani Lusekelo kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambaye ni mbobezi wa lugha za kigeni ameonesha namna wataalamu wanavyofanya tafiti zao kwa lugha za kigeni badala ya Kiswahili.

Pamoja na kuwataka watafiti kuweka kumbukumbu za lugha ya Kiswahili na kusisitiza wataalamu wa Tanzania kuanza kufanya tafiti zao kwa lugha ya Kiswahili ili nchi nyengine za Afrika waige mfano huo.

Wataalamu hao wametaka lugha ya Kiswahili ipewe hadhi sawa na lugha nyengine ili kuvisaidia vizazi vinavyokuja kupata kushuhudia thamani ya lugha yao ambayo ndio yenye kuwaunganisha waafrika.  Professa Patrick Lumumba kutoka Kenya aliituliza hadhira uliyokuwa mbele yake ikimsikiliza kwa kutumia misemo la lafdhi iliyowavutia wengi.

Kesho kumeandaliwa matembezi rasmi ya washiriki wote wa lugha ya Kiswahili na keshokutwa kutakuwa na ufunguzi rasmi wa siku ya Kiswahili duniani ambapo kilele chake kinakhitimishwa Ijumaa hiyo ya Julai saba kwa kuhudhuriwa na viongozi wa kuu wa nchi.