1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wachezaji 4 wa Czech kukosa mechi na Ubelgiji

Josephat Charo
27 Machi 2021

Vilabu vya ligi kuu ya soka ya Ujerumani vimekataa kuwaruhusu wachezaji wanne wa Jamhuri ya Czech kwenda kuichezea nchi yao mechi ya kufuzu kwa kombe la dunia dhidi ya Ubelgiji Jumamosi (27.03.2021)

https://p.dw.com/p/3rGhD
Fußball: Bundesliga I VfL Wolfsburg - Werder Bremen | Tor: 1:1
Mlindalango Jiri Pavlenka aliposhindwa kuokoa mkwaju wa Ridle Baku wa VfL Wolfsburg aliyesawazisha 1-1 katika mechi ya Bundesliga 27.11.2020, Picha: Maik Hölter/Team2/imago images

Uamuzi huo unatokana na wasiwasi kwamba wachezaji hao watalazimika kukaa karantini watakaporejea Ujerumani, aliongeza kusema, Petr Sedivy, msemaji wa timu ya taifa ya Czech, katika taarifa aliyoitoa.

Nahodha na kiungo wa timu ya Hertha Berlin, Vladimir Darida, mshambuliaji wa Bayer Leverkusen, Patrick Schick, beki wa Hoffenheim, Pavel Kaderabek, na mlindalango wa Werder Bremen, Jiri Pavlenka, wote walicheza katika kikosi cha kwanza cha mechi ya kufuzu ya kundi E siku ya Jumatano dhidi ya Estonia lakini sasa wataikosa mechi dhidi ya Ubelgiji.

Siku ya Ijumaa Ujerumani iliamua kulegeza vizuizi kwa watu wanaowasili kutoka Jamhuri ya Czech, lakini sheria mpya hazitaanza kutekelezwa hadi Jumapili, alisema msemaji wa timu ya taifa ya Jamhuri ya Czech katika taarifa yake.

"Maafisa wa Ujerumani hawakuweza kuthibitisha kwamba wachezaji hao wa timu ya taifa hawatalazimika kwenda katika karantini pindi watakaporejea Ujerumani," alisema Sdivy, akielezea kwa nini vilabu hivyo havingewaruhusu wachezaji waondoke.

"Kutokana na sababu hizi, Jiri Pavlenka, Pavel Kaderabek, Vladimir Darida na Patrick Schick watacheza tu mechi ya Jumanne huko Wales, ambayo hatua za sasa za Ujerumani zinaruhusu."

Ubelgiji pia itapungukiwa na wachezaji. Wachezaji watano wanaocheza katika Bundesliga hawatashiriki katika mechi ya kundi E kwa sababu ya vizuizi vya usafiri kwenda Jamhuri ya Czech na kutokana na majeraha wanayoendelea kuyauguza Yannick Carrasco na Thomas Vermaelen.

Jamhuri ya Czech ilianza kampeni yake ya kufuzu kwa michuano ya kombe la dunia kwa aina ya kipeke ilipoinyeshea mvua ya magolo 6-2 Estonia wiki hii huku Ubelgiji ikiichabanga Wales 3-1.

(reuters)