1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais na wabunge wa Tigray wameondolewa kinga ya kushtakiwa

12 Novemba 2020

Bunge la Ethiopia limewaondolea kinga ya kushtakiwa wabunge 39 akiwemo rais wa jimbo la Tigray Debretsion Gebremicheal. Hatua hiyo inakuja wakati mgogoro ukiendelea katika jimbo la Tigray.

https://p.dw.com/p/3lBNM
Äthiopien Getachew Reda in Addis Abeba
Getachew Reda afisa mwandamizi wa kundi la ukombozi wa watu wa Tigray TPLFPicha: DW/Y. Geberegeziabeher

Vyombo vya habari nchini Ethiopia vimeripoti juu ya hatua hiyo ya bunge leo Alhamisi ambapo pia imeelezwa kwamba miongoni mwa walioondolewa kinga hiyo ya kutoshtakiwa yumo pia Getachew Reda ambaye ni afisa mwandamizi wa kundi la ukombozi wa watu wa Tigray TPLF ambalo liko katika mapambano na vikosi vya jeshi la serikali kuu. Soma zaidi Maelfu ya wakimbizi wa Tigray wakimbilia Sudan

Waziri mkuu Abiy Ahmed amezungumza leo na kusema kwamba operesheni hiyo ya kijeshi imeikomboa sehemu ya Magharibi ya jimbo hilo la Tigray ambako wanajeshi wa serikali wamekuwa wakipambana na wanajeshi wa jimbo hilo kwa wiki nzima sasa.

Na kutokana na jimbo hilo kutengwa kabisa na ulimwengu mwingine wa nje, hakuna chombo huru kinachoweza kuthibitisha hilo au iwapo kuna jibu lolote lilotolewa mara moja na kundi la TPLF ambalo linashikilia mamlaka ya utawala wa jimbo hio la Kaskazini lenye wakaazi zaidi ya milioni 5.

Umoja wa Mataifa utaendelea kutafuta ufumbuzi

Karte Äthiopien Region Tigray EN
Ramani ya jimbo la Tigray

Umoja wa Mataifa umeelezea wasiwasi wake kuhusu mgogoro huo wa Tigray na athari zake kwa wananchi.Gutteres atoa wito wa kusitishwa mapigano Tigray, Ethiopia Na msemaji wa katibu mkuu Antonio Gutterres,Stephanie Dujarric akizungumza leo amesema Umoja huo unaendelea kutafuta ufumbuzi wa kuwalinda raia.

"UNHCR imetuambia wanashirikiana na mamlaka nchini Sudan kuwasaidia wakimbizi zaidi ya 7000 waliokimbia kutoka Ethiopia katika kipindi cha siku mbili zilizopita, bila shaka hii ni kutokana na mapigano ya Tigray. UNHCR na maafisa wa huko wanakagua na kuwaandikisha watu wanaowasili Sudan. Wakimbizi wengi kutoka Ethiopia wanatarajiwa kuwasili katika nchi za jirani.'' amesema Stéphane Dujarric.

Kadhalika mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la misaada ya kibinadamu nchini Ethiopia, Sajjad Mohammed Sajid amesema,zaidi ya raia 1000 wa nchi mbali mbali za kigeni wamekwama katika jimbo hilo la Tigray.

Wakati wasiwasi wa mgogoro huo wa Ethiopia ukizidi kusambaa nje ya mipaka ya jimbo la Tigray, serikali kuu mjini Addis Ababa imearifu kwamba imewakamata kiasi washukiwa 150 wanaotuhumiwa kutaka kuleta hofu na kufanya vitendo vya ugaidi nchini humo.

 

 

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW