1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vituo vya kupigia kura vyafungwa Kenya

9 Agosti 2022

Vituo vya kupigia kura vimefungwa Kenya baada ya uchaguzi uliodumu kutwa nzima. Wagombea watatu wa urais wamefanikiwa kupiga kura huku mgombea wa nne George Wajackoyah wa chama cha Roots akipataka hitilafu ya mitambo.

https://p.dw.com/p/4FKSN
Kenia Wahlen 2022
Picha: Patrick Meinhardt/AFP

Wakati huo huo Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka IEBC imefutilia mbali madai kuwa mashine za kuwatambua wapiga kura zimeshindwa kufanya kazi kwa kiasi kikubwa.

Tume ya IEBC imeshikilia kuwa ni mashine 200 pekee ambazo zilipata hitilafu wakati wa kupiga kura. Kwa mujibu wa kamishna Justus Nyan'gaya, taarifa kwamba mashine hizo za kuwatambua wapiga kura zilifeli kwa kiasi kikubwa sio sahihi.

Mashine 6 zilitolewa kila wadi

Ifahamike kuwa kila wadi ilipata mashine 6 za ziada kutumika pale matatizo yanapozuka.

Hali hiyo imeilazimu Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka IEBC kutumia daftari asilia la wapiga kura kuwatambua katika maeneo ya Makueni na Kakamega ambako mashine za mfumo wa kusimamia uchaguzi Kenya, KIEMS zilipata hitilafu za mitambo.

Kenia Wahlen 2022
Maafisa wa IEBC katika eneo la KisumuPicha: Brian Ongoro/AFP

Kwa mujibu wa naibu mwenyekiti wa tume hiyo, Juliana Cherera vituo 84 katika eneo bunge la Kibwezi na vyengine 54 vya Malava, Matungu, Mumias East na Magharibi vikipatikana na hali hiyo.

Watu milioni 6.5 waliiga kura hadi ahudhuri

Takwimu za awali zilionyesha kuwa watu milioni 6.5 walikuwa wamepiga kura ilipofika mida ya adhuhuri. Jumla ya wapiga kura milioni 22.1 waliandikishwa kushiriki kwenye zoezi hili la kihistoria.

Kwa sasa usalama umeimarishwa kwenye ukumbi wa Bomas wa Kenya ambacho ndicho kituo rasmi cha kukusanya na kujumlisha matokeo ya uchaguzi. Mshindi wa kinyang'anyiro cha urais atatangazwa kutokea Bomas. Matokeo yanaanza kupokelewa kuanzia saa 11 jioni.