1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAfrika Kusini

Viongozi wa kundi la BRICS waafikiana kuongeza wanachama

24 Agosti 2023

Viongozi wa kundi la mataifa yanayoinukia kiuchumi la BRICS wamekubaliana kuongeza idadi ya wanachama na kuidhinisha masharti kwa nchi nyingine kujiunga na kundi hilo.

https://p.dw.com/p/4VWFk
BRICS Gipfel 2023 in Südafrika
Viongozi wa mataifa ya kundi la BRICSPicha: Alet Pretorius/REUTERS

Uamuzi huo umefikiwa wakati wa siku ya pili ya mkutano wa kilele unaofanyika nchini Afrika Kusini.

Hayo yameelezwa na maafisa wanaohudhuria mkutano huo wa mjini Johannesburg ikiwemo Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Afrika Kusini, Naledi Pandor.

Mwanadiplomasia huyo amesema viongozi wa BRICS, wameridhia kuyakaribisha mataifa mengine ndani ya kundi hilo na tangazo rasmi la hatua hiyo litatolewa kabla ya kufungwa kwa mkutano huo leo Alhamisi.

Miito ya kutanua ukubwa wa kundi la BRICS linaloundwa na mataifa ya China, Brazil, Urusi, India na Afrika Kusini, ndiyo ilitawala ajenda za mkutano huo wa 15 wa kilele.

Duru zinasema karibu nchi 12 duniani zimeomba kujiunga na kundi la BRICS, ambalo hivi sasa linawakilisha nusu ya idadi ya watu duniani na robo  ya thamani ya uchumi wa ulimwengu.