1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vikosi vya Uganda vyaingia Congo vikiwasaka waasi

John Kanyunyu1 Desemba 2021

Wanajeshi wa Uganda wameingia katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo kupitia mpaka wa Nobili, kilomita 70 kaskazini mashariki mwa Beni, kushiriki operesheni za pamoja na jeshi la Kongo FARDC dhidi ya waasi wa ADF.

https://p.dw.com/p/43goy
Uganda UPDF Truppen Armee
Picha: Getty Images/AFP/P. Busomoke

Ilikuwa furaha na shangwe miongoni mwa wakazi wa mji mdogo wa Nobili, pale wanajeshi wa Uganda walipovuka mpaka na kuingia kwenye ardhi ya Kongo. Wakaazi hao, wanasema wanaamini kuwa mwisho wa mauaji yanayofanywa na kundi la waasi la ADF sasa unakaribia.

Kuingia Congo kwa UPDF kulikuwa kunasubiriwa kwa muda mrefu, na hasa kushambuliwa kwa ngome kadhaa za waasi kutoka Uganda ADF na jeshi la Uganda, kumeshangiliwa pia na wabunge wa mikoa ya Kivu ya Kaskazini pamoja na Ituri.

Akizungumza na DW kwa njia ya simu, mbunge Kiro Tsongo Grégoire anayeuwakilisha mji wa Beni alisema, kuwa kile walichokisubiri kwa muda mrefu kimewadia na alitumia fursa hiyo kuwaomba wakaazi wa eneo hili kuunga mkono operesheni hizo za pamoja, ambazo kwa maoni yake zitasaidia kurejesha usalama katika eneo hili, jambo litakalowapelekea wakulima kurudi katika mashamba yao.

Afrika Flucht Flüchtlinge in DR Kongo
Mashambulizi ya mashariki mwa Congo yamesababisha maelfu kukosa makaaziPicha: Getty Images/AFP/P. Moore

Vikosi vingine vya jeshi la Uganda vinavuka mpaka pamoja na vifaa vingi, ilikuendelea na operesheni kabambe zilizoanzishwa Jumanne.Congo yakanusha kukubali operesheni na jeshi la Uganda

Na wakati huo huo, jeshi la Congo nalo linaimarishwa katika eneo hili, ilikuhakikisha kwamba ADF wanatokomezwa.

Na huko hayo yakiarifiwa, jeshi la Congo lilipambana na ADF jana katika eneo la Kirsanga,kwenye barabara inayoelekea Beni kutoka kwenyi mji mdogo wa Lubiriha kwenyi mpaka na Uganda.

Katika mapambano hayo, wapiganaji watatu wa ADF waliuawa,na silaha moja ya msaada kutekwa na jeshi la Congo, alisema captain Anthony Mualushayi, msemaji wa jeshi katika operesheni Sokola1.