1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaEthiopia

Vifo baada ya maporomoko vyaongezeka Ethiopia

25 Julai 2024

Idadi ya vifo vilivyotokana na maporomoko ya ardhi nchini Ethiopia imeongezeka na kufikia watu 257.

https://p.dw.com/p/4ijjA
Äthiopien Rettungseinsatz und humanitäre Hilfe in der Gofa-Zone
Operesheni ya uokoaji baada ya maporomoko nchini Ethiopia, wakati wakisubiri misaada ya kibinadamu katika eneo la Gofa.Picha: Gofa Zone Government Communication Affairs Department

Kulingana na taarifa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Uratibu wa Masuala ya Kibinadamu (OCHA), na kuhofia kuwa huenda idadi hiyo ikaongezeka hadi watu 500.

Janga hilo lilitokea siku ya Jumatatu baada ya mvua kubwa kunyesha kwenye kijiji kidogo cha Kencho Shacha Gozdi, kilichopo eneo la milimali katika katika jimbo la Ethiopia Kusini.

Soma pia: Mashirika ya misaada yatapa kupeleka misaada kusini mwa Ethiopia

Waokoaji wanaendelea na msako wa kutafuta miili na manusura katika eneo lililokumbwa na maafa, huku umati wa wenyeji waliofadhaika wakichimba kwenye matope kwa kutumia mikono na koleo.

Shirika la masuala ya kibinaadamu la Umoja wa Mataifa, OCHA limenukuu taarifa ya mamlaka za eneo hilo,  zaidi ya watu 15,000 wanahitaji kuhamishwa kwa sababu ya hatari kubwa ya maporomoko zaidi ya ardhi, ikiwa ni pamoja na angalau watoto 1,320 walio chini ya umri wa miaka mitano na wajawazito 5,293 au kimama wenye watoto wachanga.

Soma pia: Idadi ya waliokufa kutokana na maporomoko ya ardhi Ethiopia yafikia 157

Shirika la Msalaba Mwekundu la Ethiopia limeripoti kwamba msaada umeanza kuwasili katika eneo hilo lililojitenga, ambalo ni gumu kufikiwa, ikiwa ni pamoja na lori nne za vifaa vya kuokoa maisha.

Maafisa wamesema kuwa wengi wa wahasiriwa walifunikwa kwenye maporomoko hayo baada ya kukimbilia kusaidia wengine wakati wa maporomoko ya ardhi ya kwanza, ambayo yalifuatia mvua kubwa iliyonyesha Jumapili katika eneo hilo lililo umbali wa kilomita 480 kutoka mji mkuu Addis Ababa.

Uokoaji unaendelea

Ethiopia-Maporomoko
Baadhi ya raia wakiendelea kusaidia katika uokoaji.Picha: Gofa Zone Government Communication Affairs Department

Katika picha moja zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii na mamlaka ya eneo hilo, imeonyesha makumi ya wanaume walizingira shimo ambalo viungo vya binadamu vilikuwa wazi kwenye matope.

Wanakijiji wengine walibeba miili kwenye machela ya muda huku katika hema la karibu wanawake waliomboleza wakiwa  wameketi karibu na safu ya miili iliyofunikwa kwa sanda wakati ikitayarishwa kwa mazishi.

Tseganesh Obole mmoja wa manusura ya maporomoko hayo amesema, "Nilifunikwa na matope pamoja na watu wengi, wakiwemo watoto wangu. Walichimba na kunitoa, lakini watoto wangu wanne wamekufa na bado wamefunikwa kwenye tope."

Shirika la OCHA limesema watu 12 waliopata majeraha wamepelekwa katika hospitali ya eneo hilo, huku takriban 125 wakiwa wameyahama makazi yao na kujihifadhi pamoja na wakaazi wengine wa eneo hilo. hata hivyo idadi ya waliopotea haijulikani.

Soma pia: Zaidi ya watu 50,000 wayakimbia makaazi yao Ethiopia

 

Maporomoko ya ardhi yaua mamia Ethiopia

Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametuma salamu za rambirambi kwa waathiriwa wa maafa hayo. Msemaji wa mkuu wa Umoja wa mataifa Stephane Dujarric amesema umoja wa Mataifa na washirika wake wanafanya kazi kwa karibu na Serikali, kutathmini hali ya kibinadamu ili kujua kiwango cha uharibifu na kutathmini mahitaji ya kibinadamu ya watu walioathirika.