1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUrusi

Urusi yawaomboleza waliokufa kwenye tamasha

24 Machi 2024

Urusi hii leo inaadhimisha siku ya kitaifa ya maombolezo kufuatia mauaji ya zaidi ya watu 130 kwenye jengo kulikokuwa kukifanyika tamasha.

https://p.dw.com/p/4e4Mi
Urusi, Moscow | jengo la Crocus
Watu wakiwa wamekusanyika kuweka maua na kuwasha mishumaa karibu na jengo la Crocus kulikotokea mauaji, Machi 23, 2024. Picha: Alexander Zemlianichenko/AP Photo/picture alliance

Kundi la kigaidi linalojiita Dola la Kiislamu limedai kufanya shambulizi hilo kubwa zaidi barani Ulaya na baya kabisa kutokea nchini Urusi kwa karibu miongo miwili.

Rais wa Urusi Vladimir Putin ameapa kuwaadhibu wahusika wa shambulizi hilo aliloliita la "kigaidi na la kinyama", akisema watu wanne wenye silaha waliokuwa wakijaribu kukimbilia Ukraine tayari wamekamatwa.

Hata hivyo, kwenye hotuba yake ya kwanza hadharani kuhusiana na shambulizi hilo, Putin hakurejelea tamko la IS la kudai kuhusika, huku akiilaumu Ukraine kwa kuhusika, ingawa Ukraine kupitia Rais wake Volodymyr Zelensky ikikana vikali na kumlaumu Putin kwa kujaribu kuwabebesha lawama.

Tayari watu 11 wamekamatwa, imesema idara ya usalama ya Urusi, FSB mapema leo.