1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUrusi

Urusi yaamuru wakaazi wa Kurski kuuhama mkoa huo wa mpakani

12 Agosti 2024

Urusi imeamuru kuhamishwa watu zaidi kutoka mkoa wake unaopakana na Ukraine katika wakati inapambana kurejesha udhibiti kamili baada ya vikosi vya Ukraine kuvuka mpaka na kuingia kwenye ardhi hiyo ya Urusi.

https://p.dw.com/p/4jNLi
Urusi, Kursk | Uharibifu baada ya shambulio la roketi la Ukraine
Urusi inapambana kurejesha udhibiti kamili wa Kursk baada ya vikosi vya Ukraine kuingia kwenye ardhi hiyo ya Urusi.Picha: Ilya Pitalev/Sputnik/IMAGO

Uvamizi huo wa Ukraine inatajwa kuwa operesheni kubwa zaidi ya kuvuuka mpaka iliyofanywa na nchi hiyo tangu Urusi ilipoivamia kijeshi zaidi ya miaka miwili iliyopita.

Kisa hicho kwenye mkoa wa Kursk kiliwalazimisha maelfu ya Warusi kukimbia na Moscow imekiri kwamba wapiganaji wa Ukraine wamefanikiwa kuingia umbali wa hadi kilometa 30 ndani ya ardhi ya Urusi.

Katika taarifa yake ya kila siku, wizara ya ulinzi ya Urusi imesema imefanikiwa kuvidhibiti vikosi vya Ukraine vilivyojaribu kuingia ndani zaidi ya ardhi ya Urusi kwa kutumia magari ya kivita.

Soma pia: Urusi yajibu mashambulizi ya Ukraine kwa kuanzisha operesheni ya kijeshi

Moscow imesema pia imeamuru kuhamishwa maelfu ya watu kutoka mkoa wa Kursk na kuwapeleka kwenye mkoa mwingine wa mpakani wa Belgorod.