1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN yatoa fedha za msaada wa dharura Ethiopia

15 Novemba 2021

Umoja wa Mataifa umesema Jumatatu kwamba umetoa fedha za dharura za kusaidia kutoa msaada wa kiutu wa kuokoa maisha na ulinzi wa raia waliokwama katika mgogoro unaoendelea kutokota nchini Ethiopia.

https://p.dw.com/p/42zru
Äthiopien | Vereilung von Hilfsgütern
Picha: Mulugeta Ayene/AP/picture alliance

Mkuu wa misaada wa Umoja wa Mataifa Martin Griffiths amesema ametoa jumla ya dola milioni 40 zinazokusudiwa kuongeza operesheni za dharua mkoani Tigray na kwingineko kaskazini mwa Ethiopia kunakoshughuliwa na mgogoro.

Aidha zitasaidia kwa ajili ya ukame unaoshuhudiwa kusini mwa nchi. Griffiths ambaye amerejea kutoka Ethiopia, amesema dola milioni 25 kati ya fedha hizo zimetoka kwa Mfuko wa Masuala ya Dharura wa Umoja wa Mataifa, wakati nyingine dola 15 zinatoka kwa Mfuko wa Kiutu wa Ethiopia.

Taarifa imesema katika maeneo ya Tigray, Afar na Amhara, fedha hizo zitasaidia mashirika ya misaada yanayotoa ulinzi na msaada mwingine wa kuokoa maisha kwa wale walioathirika na mzozo huo.