1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN: Wahamiaji waliokufa au kupotea baharini yaongezeka 2023

29 Septemba 2023

Umoja wa Mataifa umesema leo Ijumaa kuwa idadi ya wahamiaji wanaoelekea Ulaya, waliofariki au kupotea katika Bahari ya Mediterania msimu huu wa joto, imeongezeka mara tatu tangu mwaka jana.

https://p.dw.com/p/4Wyoj
Boti ikiwa imefurika wahamiaji
Maelfu ya wahamiaji huvuka bahari ya Mediterania kwa kutumia mitumbwi au boti za mpira.Picha: DARRIN ZAMMIT LUPI/REUTERS

Umoja huo umebainisha kuwa bahari hiyo imegeuka kuwa "makaburi" ya watoto.  

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia Watoto UNICEF, limesema kuanzia mwezi Juni hadi Agosti, takriban watu 990 walikufa au kutoweka wakijaribu kuingia Ulaya kutoka kaskazini mwa Afrika, ikilinganishwa na vifo 334 katika kipindi hicho mwaka 2022.     

Nicola dell'Arciprete, mratibu wa UNICEF nchini Italia amesema mwaka huu, takriban watoto 289 wamekufa kufikia sasa walipokuwa wakijaribu safari hizo za hatari.

Kwa mujibu wa Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuwahudumia Wakimbizi UNHCR, wahamiaji wapatao 2,500 wamefariki au kutoweka katika Bahari ya Mediterania katika kipindi cha Januari 1 hadi Septemba 24, ikiwa ni ongezeko la asilimia 50 ikilinganisha na mwaka jana.