1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulio ya Israel dhidi ya Hamas yaendelea

12 Novemba 2023

Shule ya Umoja wa Mataifa katika mji wa Gaza iliyoshambuliwa ilikuwa ikiwahifadhi watu waliokimbia vita

https://p.dw.com/p/4Yivl
Shule inayoendeshwa na UN yashambuliwa Gaza
Mtoto wa Kipalestinaakilia baada ya shule inayohifadhi wakimbizi kushambuliwaPicha: Anas al-Shareef/REUTERS

Umoja wa Mataifa umesema watu wengi wameuwawa na wengine chungunzima wamejeruhiwa katika mashambulizi yaliyofanywa dhidi ya shule moja inayosimamiwa na Umoja huo Kaskazini mwa Gaza. Shule hiyo ilikuwa ikiwahifadhi mamia ya Wapalestina waliokimbia vita.Soma pia:Umoja wa Mataifa waionya Israel juu ya kuizingira Hamas

Jumamosi Jioni shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa UNDP lilitowa taarifa likisema, mashambulizi yaliyofanywa yalisababisha vifo na majeruhi na kwamba hali hiyo haikubaliki na mauaji ya raia yanapaswa kusitishwa.

Israel imekuwa ikishambulia kwa mabomu kila mahala katika Ukanda wa Gaza tangu kundi la Hamas lilipofanya shambulio la kushtukiza kusini mwa Israel na kuuwa kiasi watu 1,200 na kuwachukuwa mateka wengine takriban 240,Oktoba 7.Soma pia:Jeshi la Israel lamshambulia kiongozi wa Hamas

Wizara ya afya ya Gaza bado haijatowa idadi ya waliouwawa katika kipindi cha saa 48 zilizopita, ikisema haijafanikiwa kuwasiliana na hospitali za eneo hilo.Wizara hiyo imesema maiti zimetapakaa mitaani huku magari ya kubeba wagonjwa yakishindwa kuzifikia maiti hizo kutokana na kuongezeka kwa mashambulizi ya mabomu na vita.

Kwengineko kiongozi wa Kanisa Katoliki Papa Francis ametowa mwito wa kuhudumiwa haraka watu waliojeruhiwa Gaza pamoja na kulindwa usalama wa raia na kutolewa msaada zaidi wa kibinadamu katika Ukanda wa Gaza.Kadhalika ametowa mwito wa kuachiliwa huru mateka na kundi la Hamas.