1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN yapongeza kuachiwa huru wafungwa nchini Libya

Saleh Mwanamilongo
1 Aprili 2021

Umoja wa Mataifa umepongeza hatua ya kuachiwa huru kwa wafungwa zaidi ya 120 nchini Libya ambao ni wapiganaji wa jenerali muasi Khalifa Haftar.

https://p.dw.com/p/3rVL5
Libyen Sirte Parlament
Picha: Libyan Prime Ministry/AA/picture alliance

Ujumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa nchini Libya, UNSMIL, unatumai kwamba hatua hiyo ni mwanzo wa maridhiano ya kitaifa nchini Libya. Ujumbe huo umepongeza juhudi za viongozi wa serikali ya muungano wa kitaifa ambayo imewaachia huru wafungwa hao wa kivita wiki mbili kabla ya kuanza kwa mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Kwa upande wake wake Waziri Mkuu wa Libya,Abdelhamid Dbeibah amesema kuwa mustakhbali na maendeleo ya Libya vitatokana na uwezo wa walibya kuponya vidonda vyao kupitia maridhiano ya kitaifa.

Wafungwa hao waliachiwa huru kufuatia hafla maalumu iliyoandaliwa na viongozi wa mji wa Zawiya, ulioko kilometa 45 magharibi mwa mji mkuu Tripoli.

Luteni kanali, Ashraf Issa, mkuu wa kitengo cha uhalifu amesema, wapiganaji hao tiifu kwa jenerali muasi Khalifa Haftar walikamatwa na wanamgambo wa mji huo wa Zawiya, baaya ya  kushindwa kwa jaribio la Haftar kuuteka mji wa Tripoli mwaka 2019.

''Walibya wanalazima yakuwa pamoja''

Libyen Demo zum Jahrestag der libyschen Revolution
Picha: Mahmud Turkia/AFP/Getty Images

Mapigano baina ya vikosi tiifu kwa serikali ya Tripoli na wapiganaji wa jenerali Haftar yali Oktoba waka jana. Na hivi sasa serikali mpya ya mpito umeundwa kwa ajili ya kuandaa uchaguzi mkuu wa Desemba.

Abdallah Ellafi naibu rais wa Libya alitoa mwito kwa ajili pande zote kupiga hatua ya mbele kwa ajili ya ujenzi wa nchi. Amesema kizazi kijacho hakitakiwi kurithi chuki na fitna kutoka kwao .

Kwa upande wake  Moussa al-Koni,makamu mwingine wa Rais amesema leo WaLibya wanalazima ya kuwa pamoja na kuungana mkono.

Zoezi la kubadilishana wafungwa litaendelea

Baraza hilo la Uongozi wa Libya, lenye wanachama watatu, liliteuliwa Februari, mjini Geneva, kufuatia mazungumzo ya pande husika chini ya uongozi wa Umoja wa Mataifa. Mwezi Machi, bunge nchini Libya liliidhinisha serikali ya Umoja inayoongozwa na waziri mkuu Abdul Hamid Dbeibah.

Wafungwa hao waliovaa kanzu na kofia nyeupe walishangiliwa na familia zao waliohudhuria hafla hiyo kwenye uwanja wa mpira wa Zawiya. Wafungwa hao wa kivita watoka miji ya Sorman na Sabratha, umbali wa kilomita 60 na 70, magharibi mwa Tripoli.

Desemba 2020  hadi Januari mwaka huu, pande hasimu zilibadilishana wafungwa kulingana na mkataba wa usitishwaji mapigano .