1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ulaya na China kushirikiana kuleta amani ulimwenguni

1 Aprili 2022

Rais wa China Xi Jinping amewataka maafisa wa ngazi za juu katika Umoja wa Ulaya kushirikiana na China katika kuutatua mzozo unaotokota nchini Ukraine.

https://p.dw.com/p/49LfR
PK EU-China-Gipfel | Ursula von der Leyen
Picha: Kenzo Triboulliard/AFP

Rais wa China Xi Jinping ametoa mwito huo wakati Umoja huo ukiangazia namna ya kuishawishi China kutoiunga mkono Urusi kwenye mzozo huo ambao unatishia kuathiri mahusiano muhimu ya kibiashaea baina ya mataifa makubwa ulimwenguni. 

Haya yamejitokeza kabla na katika mkutano wa kilele kati ya China na Umoja wa Ulaya unaofanyika kwa njia ya mtandao.

Rais Xi Jinping amemwambia Rais wa Baraza la Ulaya, Charles Michel pamoja na Rais wa Halmashauri ya Umoja huo, Ursula von der Leyen kwamba Umoja wa Ulaya na China wanatakiwa kuangazia namna za kuzuia kusambaa zaidi kwa mzozo huo, hii ikiwa ni kulingana na taarifa ya majumuisho ya mazungumzo ya faragha ya viongozi hao iliyotolewa na Balozi Wang Lutong.

Taarifa hiyo aidha imesema, Xi amesema mahusiano kati ya China na Umoja wa Ulaya yanaweza kutumika kama  chanzo cha ustahimilivu wa ulimwengu katikati ya uvamizi wa China nchini Ukraine.

Vladimir Putin und Xi Jinping
Rais wa China Xi Jinping(aliyekaa) na rais wa Urusi Vladimir Putin, aliesimama.Picha: Pavel Golovkin/Pool/REUTERS

Mapema, Umoja wa Ulaya ulikuwa ukiangazia namna ya kuishawishi China kutoiunga mkono kwa namna yoyote Urusi katika mzozo huo unaotishia kuathiri mahusiano ya kibiashara baina ya mataifa yenye nguvu kubwa ya kiuchumi ulimwenguni.

Michel na von der Leyen kabla ya kuzungumza na rais Jinping, walikutana kwanza na waziri mkuu wa China Li Keqiang, na kulingana na taarifa mazungumzo yao yalikuwa ni ya kuangazia masuala ya bishara na mabadiliko ya tabianchi, ingawa hata hivyo yaligubikwa na wasiwasi wa magharibi kuhusiana na uungaji mkono wa China kwa Urusi katika mzozo huo wa Ukraine.

Soma Zaidi: Marekani, washirika wazidisha shinikizo la kiuchumi kwa Urusi

China yasema itatumia njia zake kusaka amani nchini Ukraine.

Msemaji wa wizara ya mambo ya kigeni wa China, Zhao Lijian aliwaambia waandishi wa habari kwamba kwenye mazungumzo hayo, Keqiang aliwaambia viongozi hao wa Ulaya kwamba China itaamua njia zake yenyewe za kusaka amani nchini Ukraine baada ya Brussels kuishinikiza kutoa uhakikisho kwamba haitaisaidia Urusi kwa kuipatia silaha ama kuvikwepa vikwazo vya magharibi.

"Kuhusiana na suala la Ukraine, ningependa kusisitiza dhamira ya China ya kuwa na sera huru ya mambo ya nje ya amani na itatoa uamuzi wake kwa kuzingatia umuhimu wa suala hilo. Mbali na hayo, nchi zote zina haki zao za kujitegemea kuamua sera zao za kigeni. Hazipaswi kuwalazimisha wengine kuchukua upande au kuchukua mtazamo rahisi wa 'rafiki au adui' au 'mweusi au nyeupe'. China na nchi nyingine ikiwa ni pamoja na zinazoendelea, zina msimamo sawa kuhusu suala hili." alisema Lijian.

Umoja wa Ulaya unahofia kwamba kushindwa kwa China kulaani uvamizi wa Urusi nchini Ukraine, kunamaanisha kwamba huenda iko tayari kuisaidia Urusi na mzozo wa kibinaadamu nchini humo.

Soma Zaidi: Viongozi wa dunia wailaani Urusi kuhusu Ukraine

Balozi Lutong ambaye pia ni mkuu wa mahusiano ya Ulaya katika wizara hiyo ya mambo ya nje ya China amesema pande hizo mbili zimekubaliana kushirikiana ili kurejesha amani, utulivu na ustawi kote ulimwenguni.

Mashirika: AFPE/DPAE/RTRE