1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ukosefu wa rutuba ya udongo watatiza wakulima Afrika

Angela Mdungu
24 Julai 2024

Matatizo ya ukosefu wa rutuba ya udongo unaotumika kwa kilimo yanazidi kuongezeka huku bara la Afrika likipambana kujikimu kwa chakula. Wakulima barani humo wanasema kuwa ardhi yao inapoteza uwezo wa kuzalisha mazao.

https://p.dw.com/p/4iggH
Kilimo cha kisasa Namibia
Kilimo cha kisasa NamibiaPicha: DW

Afrika ina asilimia 65 ya ardhi yenye rutuba ambayo haijalimwa iliyosalia kote duniani. Licha ya ukweli huo, benki ya maeneleo ya Afrika inabainisha kuwa bara hilo linatumia karibu dola bilioni $60 kila mwaka kununua chakula kutoka nje.Wadau wajadili kilimo cha kulinda mazingira mjini Kampala

Matumizi hayo yanatarajiwa kuongezeka hadi kufikia dola bilioni $110 utakapofika mwaka 2025 kutokana na ongezeko la mahitaji pamoja na mabadiliko ya mwenendo wa watumiaji.  Kulingana na Wizara ya Kilimo ya Kenya, karibu asilimia 63 ya ardhi yenye rutuba nchini humo ina tindikali.

Kwa upande wake Shirika la Chakula na Kilimo duniani linaripoti kuwa uzalishaji wa mahindi ulipungua kwa asilimia 4.4 mwaka 2022. Hata hivyo halikutaja sababu.

Kilimo-Namibia
Kilimo nchini Namibia Picha: DW

Benson Wanjala  ni mkulima katika kijiji kimoja magharibi mwa Kenya. Anasimulia kuwa,  alipoanza shughuli za kilimo zaidi ya  miongo miwili iliyopita, shamba lake la ekari 10 lilikuwa na uwezo wa kuzalisha magunia 200 ya mahindi. Sasa anapata magunia 30 pekee.

Analalamika kuwa, ardhi yake iliyokuwa na rutuba haina uhai tena na haimsaidii kuendesha maisha kama hapo awali hivyo imempasa kuangalia namna nyingine ya kuishi.Afrika yashauriwa kukuza kilimo cha kisasa

"Nilishauriwa kutumia mbolea, lakini sikuwa nafuga ng'ombe wakati huo. Wakati nikiwa najiuliza ni kwanini uzalishaji wa mazao umepungua, niliamua kuhamia Nairobi na kuanza kulima mbogamboga," alisema mmoja wa wakulima.

Wizara ya ardhi ya Kenya haikujibu maswali juu ya changamoto hii hasa mara baada ya kashfa ya mwezi Aprili kuhusu uwepo wa mbolea ya uwongo. Mbolea hiyo ilipatikana katika mifuko iliyoandikwa majina bandia na kugawanywa kwa wakulima kupitia programu maalumu ya ruzuku ya kitaifa. 

Soma: Umoja wa Mataifa waonya juu ya athari za mabadiliko ya hali ya hewa katika mashamba na kaya za vijijini zinazoendeshwa na wanawake katika nchi maskini

Rais William Ruto alisema kuwa wakulima wasiopungua 7,000 walinunua mbolea hiyo na wangepewa fidia kwa kupatiwa mbolea sahihi. Mwezi Mei, nchi hiyo ilikuwa mwenyeji wa mkutano wa kilele wa afya ya udongo barani Afrika pamoja na masuala mengine yanayolenga kuongeza uzalishaji wa chakula.

Katka Mkutano huo Mkurugenzi mtendaji wa chama cha wakulima wa Afrika Mashariki Stephen Muchiri, alitoa wito kwa wakulima kurejea katika njia za asili za kilimo.

Kwa nini Afrika lazima iimarishe kilimo cha kisasa ?

Kwa upande wake mwanaharakati wa masuala ya chakula katika shirika la Greenpeace Afrika Elizabeth Atieno Opolo, amesema wakulima hawana budi kujikita kwenye kilimo endelevu. Anaongeza kuwa licha ya kuwa kilimo cha aina hiyo kinachukua muda mrefu, manufaa yake ni ya muda mrefu pia. Ameongeza kuwa, matumizi ya mbolea za kemikali si tu kuwa yanaharibu ardhi bali pia yanaangamiza kabisa mazingira kwa ujumla.

Soma pia: Jukwaa la Mfumo wa Chakula Afrika lahitimishwa Tanzania

Kuporomoka kwa ubora wa ardhi ya kilimo si tatizo la Kenya pekee bali ni changamoto inayotia wasiwasi usalama wa chakula kote Afrika. Nchini Zimbabwe, asilimia 70% ya udongo una tindikali, kwa mujibu wa serikali. Kipindi cha nyuma, serikali ya taifa hilo ilileta mbolea za kemikali katika juhudi za kuimarisha udongo. Hata hivyo matumizi mabaya ya mbolea hizo yalikwamisha malengo.

Shirika linalopigia upatu mageuzi ya Kilimo barani Afrika la AGRA linapendekeza wakulima wapime tindikali katika udongo wao na watumie chokaa ili kupunguza kiwango kikubwa cha kemikali hiyo. Lakini wakulima wanasema gharama ni kubwa. Kupima udongo kunagharimu dola  $20 hadi $40 za kimarekani.